Tuesday, January 19, 2016

TUNDURU YAPOKEA MILIONI 129.1 KWA AJILI YA KUBORESHA ELIMU



Na Steven Augustino,
Tunduru.

JUMLA ya shilingi milioni 129,125,000 zimepokelewa wilayani Tunduru, mkoa wa Ruvuma ili zeweze kutumika katika shughuli za utoaji wa elimu bure kulingana na ahadi iliyotolewa na Rais wa awamu ya tano, Dkt. John Pombe Magufuli. 

Hayo yalisemwa na Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Agnes Hokororo wakati alipokuwa akizungumza hivi karibuni na wataalamu wake katika kikao cha kazi kilichofanyika ukumbi wa Klasta ya walimu wa tarafa ya Mlingoti mjini hapa.

Aidha Hokororo  aliwatahadharisha watendaji hao kwamba fedha hizo ni za moto, unaowaka na kiongozi atakayejidai kuchakachua ajiandae kuunguzwa na moto huo.

Katika kikao hicho Mkuu huyo wa wilaya alikuwa akizungumza na wakuu wa idara za halmashauri ya wilaya hiyo, wakuu wa shule za sekondari 21 na msingi, waratibu elimu kata ambao pia alikuwa anawapa maelekezo hayo juu ya matumizi ya fedha hizo.


Alisema kwa mwaka huu, wilaya yake tangu ianzishwe mwaka 1905 imepokea fedha nyingi tofauti na miaka iliyopita.

Hokororo alitumia nafasi hiyo kwa kuwataka watumishi wake, kusimamia ipasavyo maelekezo wanayopewa na serikali ili kuweza kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Katika maelekezo hayo pia aliwataka watumishi hao kwenda kutoa maelekezo ya kina kwa wazazi na walezi wa watoto hao, ili kuwaondolea dhana potofu ambayo inaonekana kujengwa kuwa elimu bure itaweza kuwanunulia hadi sare za watoto hao jambo ambalo sio la kweli.

Naye Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Tunduru, Tina Sekambo aliwasihi watumsihi hao kufanya kazi za utumishi wa umma kwa uwazi ikiwa ni pamoja na kubandika taarifa za mgawanyo na matumizi ya fedha zote, zinazopokelewa katika shule zao.

No comments: