Thursday, January 14, 2016

UCHANGIAJI WA CHAKULA SONGEA WAZAZI WAZUA MZOZO



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

KITENDO cha kusitisha zoezi la Wazazi kuchangia chakula, kwa shule za sekondari za kutwa za serikali zilizopo katika Manispaa ya Songea mkoani humo baadhi ya Wakuu wa shule hizo wamesema kwamba, ni ukiukwaji wa maagizo yaliyotolewa na serikali kupitia mwongozo wake uliosambazwa katika mikoa yote hapa nchini.

Aidha kufuatia hali hiyo shule hizo ambazo sasa zimefunguliwa na kuanza muhula wa masomo Januari 11 mwaka huu, nimeshuhudia watoto wakikosa chakula shuleni huku wakilazimika kuhudhuria vipindi vya masomo darasani bila kula chakula, kuanzia majira ya asubuhi hadi saa 10:00 jioni wanaporejea majumbani kwao.

Ukiukwaji huo wa agizo la serikali, wanasema kuwa unathibitisha kufuatia mwongozo uliotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Novemba 23 mwaka jana (nakala tunayo) wenye kumbu kumbu namba DC. 297/507/01/146 katika kipengele cha 4 ukielekeza kwamba majukumu ya mzazi ni pamoja na kuhakikisha kwamba huduma ya chakula kwa wanafunzi wa kutwa anachangia, yakiwemo na mahitaji mengine ya kibinadamu kama vile sare za shule na michezo, matibabu, vifaa vya kujifunzia ikiwemo daftari na kalamu.


Vilevile mzazi akiwa sehemu ya mwananchi na jamii inayozunguka shule husika, atashiriki kikamilifu katika kazi ya ujenzi wa miundombinu ya shule kwa kuchangia nguvu zao kadri itakavyoamriwa na mkutano husika wa kijiji, mtaa, kata au tarafa.

Uchunguzi wa mwandishi wetu umebaini kwamba, sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014 na ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2015 hadi 2020 ibara ya 52 (a) imebainisha kwamba serikali itatoa elimu bure kwa ngazi ya elimu awali, msingi hadi kidato cha nne bila malipo ya ada na michango mingine ya uendeshaji wa shule kuanzia mwaka wa masomo wa 2016, lakini haitamki kwamba mzazi asichangie chakula cha mtoto wake shuleni kwa shule hizo za kutwa.

Serikali kuu na mamlaka za serikali za mitaa zitaendelea kugharimia uendeshaji wa shule, kwa kutoa ruzuku na fedha ya chakula kwa shule maalumu za msingi na sekondari za bweni na sio zile za kutwa, kugharimia pia taaluma, madawati na ukamilishaji ujenzi wa majengo ya shule.

Pia walimu hao wa shule za sekondari za kutwa katika Manispaa ya Songea nimezungumza nao kwa nyakati tofauti, wameeleza kuwa usitishaji wa mchango wa chakula kutoka kwa wazazi ni agizo lilitolewa na Ofisa elimu wa sekondari mkoani humo, Mayasa Hashim kwani wao walikwisha andaa na kufuata utaratibu wa mzazi kuchangia chakula kadri ya mwongozo huo uliotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusiana na shule hizo hapa nchini zinavyopaswa kuchangia.

Walisema kuwa kufikia Disemba 21 mwaka jana, wakuu wa shule za sekondari katika Manispaa hiyo wote waliitwa na kupewa mwongozo huo uliotolewa na TAMISEMI huku wakisisitizwa kufuata yaliyomo ndani yake.

“Baada ya kupewa tuliambiwa na kusisitizwa tufuate yaliyomo katika mwongozo huu, wakuu wa shule wote tulifanya hivyo tunachotambua michango na ada imefutwa lakini chakula kwa shule za kutwa mzazi lazima achangie”, walisema.

Hata hivyo alipohojiwa na waandishi wa habari ofisini kwake, Ofisa elimu wa shule za sekondari mkoa wa Ruvuma Mayasa Hashim alikiri kusitisha kwa mchango wa chakula na michango mingine kutoka kwa wazazi, huku akiongeza kuwa utaratibu mwingine unaandaliwa na tayari wakuu wote wa shule za sekondari za kutwa katika Manispaa hiyo, wamepewa maelekezo ya kufanya juu ya suala hilo.

No comments: