Thursday, April 16, 2015

MUNDAU: FRELIMO ITAENDELEA KUDUMISHA USHIRIKIANO WETU

Na Kassian Nyandindi,
Nyasa.

IMEELEZWA kuwa ushirikiano uliopo kati ya wananchi wa vijiji vya Lunyere kilichopo wilayani Nyasa nchini Tanzania na Mpapa wilaya ya Lagunyasa jimbo la Lichinga Msumbiji, umetakiwa kudumishwa ili amani na utulivu uliopo mpakani kati ya nchi hizo mbili uweze kuendelea.

Hayo yalisemwa na Kamanda wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) wilayani humo, Cassian Njowoka alipokuwa akizungumza na wananchi mara baada ya kumwapisha kamanda wa jumuiya hiyo kata ya Mpepo Bosco Kihwili, sherehe ambayo ilifanyika katika kijiji cha Lunyere.

Njowoka alisema wananchi wa Lunyere, hususani vijana wamekuwa wakijihusisha na shughuli za uchimbaji madini ambapo kutokana na uhusiano  mzuri uliopo kwa muda mrefu baina ya nchi hizo mbili, wengi wao wamekuwa wakivuka mpaka na kwenda Msumbiji ambako pia hufanya shughuli za uchimbaji bila kikwazo hivyo ni vyema wakazingatia sheria zilizopo ambazo zinapaswa kufuatwa pindi wanapotaka kuingia nchi hiyo jirani.


Alisema kuwa ameelezwa kwa muda mrefu viongozi wa vijiji hivyo, wamekuwa wakitembeleana na kusaidiana katika shughuli za kimaendeleo na kwamba hata imefika wakati kujenga undugu kati ya wananchi wa vijiji hivyo.

“Nimefurahi sana leo, kuona viongozi wa kijiji jirani cha Msumbiji kualikwa katika sherehe hizi hii inaonesha wazi uhusiano ambao umedumu kwa muda mrefu kati yenu unaendelezwa, kama ulivyoasisiwa na viongozi waasisi wa nchi hizi”, alisema Njowoka.

Akizungumza katika sherehe hizo mara baada ya kupewa nafasi, Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Mpapa nchini Msumbiji, Alexandria Mundau Kosa alisema dhamira ya chama chao cha FRELIMO ni kuendelea kudumisha ushirikiano huo baina ya nchi hizo na kwamba aliwapongeza viongozi wa juu wa pande hizo mbili, kwa kuendeleza mahusiano hayo ambayo yalikuwepo kabla hata ya nchi hizo kupata uhuru.

Mundau Kosa alipongeza jitihada zinazoendelezwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) na serikali yake kwa kufungua mipaka, ikiwemo ujenzi wa barabara ambao unaziunganisha kitendo ambacho imeelezwa kuwa, kitasaidia wananchi wa pande hizo kunufaika kwa namna moja au nyingine.


Kadhalika Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Lunyere, Anderson Haulle alisema wataendelea kudumisha ushirikiano huo ili wananchi wake waishi kwa amani na utulivu na kwamba hawatakuwa na suluhu, kwa wale ambao watajitokeza kuleta vurugu au uvunjifu wa amani ambayo mwisho wake itasababisha kuzorotesha mahusiano mazuri yaliyopo kati yao.

No comments: