Wednesday, April 1, 2015

TAMKO LA MAASKOFU NA WACHUNGAJI KUTOKA MADHEHEBU MBALIMBALI JUU YA TUKIO LA ASKOFU GWAJIMA

SISI maaskofu na wachungaji kutoka makanisa mbalimbali tumeshtushwa na kusikitishwa kwa taarifa ya ugonjwa wa Askofu na mtumishi mwenzetu Josephat Gwajima ambaye tarehe 27/03/2015 alifika kituo cha polisi cha kati kuitikia wito wa polisi uliomtaka kwenda kujibu shutuma za kutumia lugha ya matusi kwa kardinali Pengo.

Tumepata fursa ya kutafakari na kujadili kwa kina hali iliyompata Askofu mwenzetu hasa baada ya kuzingatia kuea Askofu Gwajima alifika polisi akiwa mzima na mwenye afya njema lakini wakati wa akihojiwa na polisi, hali yake ilibadilika ghafla kiasi cha kupelekea yeye kulazwa hospitali ya TMJ akiugua tena kwenye wodi ya wagonjwa mahututi yaani (ICU) katika chumba cha uangalizi maalum.

Maswali yetu makuu ni kitu gani kimempata mwenzetu? Tunajiuliza, je vyombo vya usalama vimekua sio sehemu salama kama zamani?

Tukiwa bado tunatafakari hill, tumeshtushwa tena baada ya kupata taarifa ya kuwa Wachungaji Wasaidizi wa Askofu Gwajima pamoja na walinzi wake waliokuwepo hospitalini hapo kwa ajili ya kumuuguza nao pia wamekamatwa kwa tuhuma za. kutaka kumtorosha Askofu Gwajima. 


Jambo hili linashangaza zaidi maana wachungaji wale wale waliokuwa naye akiwa mzima wa afya wakati anaelekea polisi ndio wale wale wanatuhumiwa kutaka kumtorosha akiwa mgonjwa.

Ni jambo la kushangaza na lisiloingia akilini kuwa wasaidizi hao wa Gwajima walitaka kumtorosha wakati Gwajima kama angekua na nia hiyo angekwisha fanya hivyo mana alikuwa na uwezo wa kutoroka alipokua Arusha kwenye kikao cha Maaskofu wakuu wa makanisa ya Kipentekoste ambao alipata taarifa za kuitwa Polisi.

Isitoshe Gwajima aliitija wito na kwenda polisi mwenyewe kwa miguu yake bila kushurutishwa, wala hakufikishwa polisi kwa nguvu.

Swali: Kama alikua anaona ugumu wa kutoroka wakati hakuna polisi anayemlinda na huku akiwa mwenye afya tele, itakuaje rahisi kutoroshwa leo akiwa mahututi na akiwa kwenye ulinzi mkali wa polisi? Mbona hii inastaajabisha?

Jambo jingine linalotupa shida ni kuhusu mlalamikaji wa kesi hii inayomkabili Askofu Gwajima. Tumeelezwa na wasaidizi wa Askofu Gwajima kuwa pale polisi walielezwa kuwa aliyefungua kesi hii sio Pengo ila mtu mmoja aitwaye Aboubakar.

Kwa ufahamu wetu juu ya sheria unatutuma kuamini kuwa Aboubakar sio MTU sahihi wa kufungua kesi hiyo sababu hawezi kutuonyesha ameumizwa kiasi gani na matamshi ya Askofu Gwajima.

Isitoshe, Kardinali Pengo mwenyewe ametamka katika Ibada yake ya Jumapili hii ya tarehe 29/03/2015 kuwa amemsamehe Gwajima, yupi tena mwenye uchungu wa kumzidi Kardinali Pengo?

RAI YETU:

Rai yetu ni kwamba, ni vizuri serikali pamoja na vyombo vyake vya usalama vikatumia weledi katika kushughulikia mambo ya kidini na viongozi wake kwani yanaweza kusababisha chuki dhidi ya serikali na pia kupelekea mpasuko mkubwa wa kidini katika jamii yetu iliyo na historia nzuri ya umoja na mshikamano na ushirikiano katika matukio yote ya kimaisha.

Tunaomba serikali isaidie kuondoa mkanganyiko huu na busara kubwa itumike ili kuepusha uvunjifu wa Amani katika jamii.

MAAMUZI YETU:
Hili linazungumzika, maana hata hivyo tumeshaazimia kukutana na IGP ili kupata suluhisho juu ya jambo hili.

Kwa niaba ya maaskofu na wachungaji:

Mwenyekiti: Askofu Dr. Mgullu Kilimba

Katibu: Askofu Dr. Dramas Mukassa

Na mwandishi;
F.A.K
30/03/2015

No comments: