Sunday, April 5, 2015

TUNDURU WAPITISHA MAKISIO YA KUNUNUA TANI 300 ZA KOROSHO

Na Steven Augustino,
Tunduru.

WANACHAMA wa chama cha ushirika wakulima wa korosho, Litungunru AMCOS katika kijiji cha Mchoteka Wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, kimepitisha bila mabadiliko makisio ya kununua tani 300 katika msimu wa kununua zao hilo kwa mwaka 2015/2016.

Maamuzi hayo yalifikiwa na wanachama hao, kwenye mkutano mkuu uliofanyika kwenye ukumbi wa ghala la wakulima wa chama hicho kijijini humo, ambapo pamoja na mambo mengine walipitisha mapato na matumizi ya mradi wa mazaowenye thamani ya shilingi milioni 480,000,000.

Aidha katika mkutano huo, wanachama waliupatia meno na kuuagiza uongozi wao kuwa wakali katika utendaji na kuangalia uwezekano, wa kuwafuta uanachama wajumbe ambao wamekuwa hawajishughulishi na uzalishaji wa korosho, au kumaliza hisa zao kwa muda mrefu na hivyo kukihujumu chama katika mapato.


Taratibu za kuwatimua uanachama wajumbe ambao hawatimizi taratibu za msingi ndani ya chama, ziliibuliwa na Ally Ambali ambapo alifafanua kuwa endapo chama kitaendelea kuwafuga watu wa namna hiyo, ipo hatari ya kufilisika.

Sambamba na maagizo hayo waliiagiza bodi yao, kuwachukulia hatua za kisheria Mohamed Matoto, Said Rashi na Msusa Daimu ambao wametimuliwa uongozi ndani ya chama kutokana na kufuja shilingi milioni 1.8 zilizotokana na ushuru wa manunuzi ya mazao mchanganyiko, kipindi cha msimu wa mwaka 2014/2015.

Walisema kuwa pamnoja na deni hilo, viongozi hao wanatuhumiwa kuweka rehani mali za chama ikiwemo mizani zenye thamani ya shilingi milioni 5.9 kwa mfanyabiashara binafsi, akiwa anawatuhumu kumwibia shilingi milioni 10,473,590 zilizodaiwa kupotea wakati wakimnunulia mazao mchanyiko katika msimu huo.

Awali akitoa taarifa hiyo, mwandishi mkuu wa chama Dauda Hassan Dauda chama chake kimefikia maamuzi ya kuongeza makisio hayo, ikiwa pia ni lengo la kuongeza mapato yake ya ndani.

Alisema chama kimefikia kuongeza makisio hayo, kutoka tani 200 ambazo kilikusanya kutoka kwa wanachama wake na kuziuza katika msimu uliopita wa mwaka 2014 hali ambayo ilikifanya kupata shilingi milioni 11,942,500 fedha ambayo ni kidogo ikilinganishwa na idadi ya wanachama na wakulima wa zao hilo waliopo sasa.

Dauda alisema endapo chama kitafanikiwa kuzalisha kulingana  na makisio hayo, kitakuwa kimeongeza mapato yake kutoka shilingi milioni 11.942 za mwaka jana na kufikia shilingi milioni 34,900,000.

No comments: