Thursday, April 30, 2015

MBIO ZA MWENGE RUVUMA KUZINDUA MIRADI YENYE THAMANI YA SHILINGI BILIONI 10.3

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dokta Alli Mohamed Shein akikabidhi Mwenge wa uhuru kwa mmoja wa wakimbiza Mwenge kitaifa, jana mara baada ya kuzindua mbio hizo katika uwanja wa Majimaji mjini Songea mkoani Ruvuma.


Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu akikabidhi Mwenge wa uhuru kwa Mkuu wa wilaya ya Songea mkoani humo, Profesa Norman Sigalla kwa ajili ya kuanza mbio zake katika wilaya ya Songea.
Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dokta Alli Mohamed Shein amekemea kitendo kinachofanywa na baadhi ya watu kuwagawa Watanzania, jambo ambalo linahatarisha amani ya nchi yetu.

Dokta Shein alisema kumekuwa na makundi ambayo huwagawa kwa misingi ya dini, rangi na ukabila jambo ambalo amekemea vikali na kutaka hali hiyo iachwe mara moja.

Vilevile alikemea vitendo vya biashara ya madawa ya kulevya, ambapo alieleza kuwa kundi la vijana ndilo kwa kiasi kikubwa linahusika na vitendo hivyo na kuwataka waachane na tabia hiyo badala yake wafanye shughuli za kimaendeleo, kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Rais huyo alifafanua kuwa ni aibu kwa taifa hili vijana kujihusisha na biashara hiyo, kwani wao ndio nguvu kazi katika kusukuma gurudumu la maendeleo hivyo serikali itaendelea kupambana na vitendo hivyo vya uuzaji wa madawa hayo, ili visiweze kuendelea.


Alisema yote hayo yanatokana na kundi hilo la vijana, kuwa na tamaa ya kutaka kupata utajiri kwa uharaka na njia zisizo halali.

“Ninawaomba Watanzania wenzangu kila mmoja wetu pale alipo akae na kutafakari, kwa kukemea kwa nguvu zote juu ya biashara hii ya madawa ya kulevya hasa kuwafichua wale wanaofanya ili tuweze kuondokana na hali ya kuliabisha taifa letu”, alisema.

Pia Shein amewataka wakimbiza Mwenge, kutoa ujumbe kwa wananchi ipasavyo kwani wao taifa limewaamini katika kutekeleza jukumu hilo muhimu.

Kwa upande wake, Waziri wa habari, utamaduni na michezo, Dokta Fenera Mkangara alisema mbio hizo za Mwenge ni tunu ya taifa na zimekuwa zikisaidia kuelimisha jamii kwa makundi yote, na kuitaka janmii kutumia haki yao ya kidemokrasia katika kupiga kura kwenye katiba ijayo na uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka huu.

Naye Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu mara baada ya kukabidhiwa Mwenge huo alisema utakimbizwa katika mkoa huo kuanzia Aprili 29 hadi Mei 4 mwaka huu, ambapo ukiwa mkoani humo utaweza kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo, kuweka mawe ya msingi na kuzindua miradi 41 yenye thamani ya shilingi bilioni 10.3 katika wilaya tano za mkoa huo.


Hata hivyo ameitaja miradi itakayokaguliwa, kuwekewa mawe ya msingi na kuzinduliwa kuwa ni ya sekta ya maji, afya, maliasili, miundombinu, elimu na kilimo ambapo Mwenge huo wa uhuru ameanza kukimbizwa mkoani Ruvuma katika Halmashauri ya Songea na baadaye kuelekea wilaya ya Mbinga.

No comments: