Thursday, April 30, 2015

OFISA USALAMA WA TAIFA ALETA KIZAZAA KWENYE UZINDUZI WA MWENGE WA UHURU KITAIFA RUVUMA

Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo Dokta Fenera Mukangara kushoto akimuongoza Rais wa Zanzibar Dokta  Alli Mohamed Shein, kwenda kuzindua mbio za Mwenge wa uhuru jana, katika uwanja wa michezo wa Majimaji mjini Songea mkoani Ruvuma. (Picha na Muhidin Amri)
Na Mwandishi wetu,
Songea.

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, Waandishi wa habari mkoani Ruvuma jana wamejikuta wakifanya kazi katika mazingira mgumu, baada ya mmoja wa Ofisa kutoka idara ya usalama wa taifa hapa nchini, kuwazuia waandishi hao wasitekeleze majukumu yao ya kazi ipasavyo.  

Ofisa usalama huyo aliwazuia wasiweze kupiga picha, na kuandika taarifa za uzinduzi wa Mwenge wa Uhuru kitaifa, zilizofanyika jana kwenye uwanja wa Majimaji mjini Songea mkoani Ruvuma.

Aidha aliwashangaza waandishi hao pale alipofikia hatua ya kutamka kwamba wasitekeleze majukumu yao ya kazi, mpaka mgeni rasmi Dokta Alli Mohamed Shein atakapokwenda kuketi jukwaani jambo ambalo wanahabari hao walimpuuza na kutumia mbinu mbadala katika kuandika habari, na kupiga picha za tukio hilo.


Kadhalika Ofisa usalama huyo alionekana kutaka kuvunja maadili yake ya kazi hasa pale, alipofikia hatua ya kuwafokea waaandishi hao na kuwaambia kwamba atawadhalilisha kwa kuwaweka mahabusu kama hawataondoka katika eneo la tukio hilo la Mwenge.

Vilevile aliendelea kuonesha dharau akiwaambia kwamba haoni wanachokifanya, hivyo waondoke haraka kabla hajachukua hatua ya kuwaita askari polisi ili watiwe nguvuni kama alivyokusudia kitendo ambacho waandishi waliendelea kumpuuza na kufanya kazi zao kama kawaida.

Mwandishi wa habari Crecensia Kapinga ambaye anaandikia gazeti la Majira, licha ya kuingilia kati na kumweleza ofisa usalama huyo kwamba hao anaowafukuza ni waandishi wa habari, bado alionekana kutomwelewa  huku akimjibu kwamba yeye hatambui kazi zao na waondoke mara moja kabla hajawaitia polisi.


Pamoja na mambo mengine waandishi wa habari mkoani hapa, wamelaani kitendo hicho kilichofanywa na ofisa huyo wa serikali, na kutaka vitendo vya kuzuia waandishi kufanya kazi zao kwa uhuru viachwe mara moja kwani tasnia ya habari nayo inamchango mkubwa katika taifa hili.

No comments: