Friday, October 24, 2014

ASKARI WA USALAMA BARABARANI MBINGA ASWEKWA MAHABUSU KWA KUMJERUHI DEREVA WA PIKIPIKI




Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

JESHI la Polisi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, limeingia katika kashfa mpya kufuatia askari wake wa usalama barabarani kumjeruhi mwendesha pikipiki kwa kumchoma na kitu chenye ncha kali kichwani, na kumsababishia jeraha ambalo lilisababisha dereva huyo kutokwa na damu nyingi.

Tukio hilo lilitokea Oktoba 20 mwaka huu majira ya mchana, eneo la stendi ya magari ya abiria mjini hapa, ambapo askari huyo anayejulikana kwa jina la Msafiri Kilango, ndiye aliyefanya kitendo hicho kwa kumchoma kichwani dereva wa pikipiki aitwaye Erick Shonga.

Kufuatia tukio hilo hali ilibadilika mjini hapa ambapo kundi la waendesha pikipiki liliandamana kuelekea kituo kikuu cha polisi cha wilaya hiyo, kwa lengo la kupinga kitendo alichofanyiwa mwenzao.

Walipofika kituoni hapo walieleza malalamiko yao wakisema kuwa askari wa usalama barabarani wilayani hapa, wamekuwa na mazoea ya kuwanyanyasa mara kwa mara waendesha pikipiki hivyo wamechoshwa na hali hiyo.

“Sisi tumechoshwa na unyanyasaji huu ambao tunafanyiwa na hawa askari, muda mwingi wakitukamata wanatupiga faini wanachukua hela zetu halafu stakabadhi ya malipo halali hatupewi”, alisema Thito Mhina mmoja kati ya madereva hao wa pikipiki.

Aliyechomwa atoa ushuhuda:

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi dereva wa pikipiki aliyejeruhiwa Erick Shonga alisema, amepatiwa matibabu katika hospitali ya wilaya hiyo ambapo ameshonwa nyuzi tatu kichwani katika eneo ambalo alichomwa na kitu chenye ncha kali kichwani.

Saturday, October 18, 2014

TANROADS RUVUMA UTATA MTUPU, YANYOSHEWA KIDOLE KWA KUJENGA BARABARA KIWANGO CHA CHINI

Barabara iliyojengwa kilometa moja, kwa kiwango cha lami eneo la Mbinga mjini mkoani Ruvuma, tabaka lake la juu likiwa limebomoka ambapo mwanzo wa barabara hiyo hadi mwisho wake katika maeneo tofauti imebomoka kwa mtindo huu, kwa kile kinachoelezwa kuwa kutokana na kujengwa kwa kutokidhi viwango husika, ambapo barabara hiyo ujenzi wake unafanywa na kampuni ya FEI - MAC LTD kutoka mjini Songea na kusimamiwa na Wakala wa barabara Tanzania (TANROADS) mkoani hapa.


Kibao hiki kinaonyesha Mkandari husika aliyefanya kazi ya ujenzi wa barabara hiyo. (Picha zote na Kassian Nyandindi)
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WAKALA wa barabara Tanzania (TANROADS) mkoani Ruvuma, ameshushiwa lawama nzito kwa kushindwa kusimamia kikamilifu ujenzi wa barabara kiwango cha lami katika eneo la Mbinga mjini mkoani humo, kutokana na barabara ambayo imejengwa na wakala huyo kuanza kubomoka tabaka la juu kabla ya kukabidhiwa rasmi mikononi mwa serikali.

Barabara hiyo ambayo ujenzi wake ni wa kilometa moja, inagharimu kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni moja  na kwamba utekelezaji wake upo chini ya usimamizi wa wakala huyo.

Malalamiko hayo yalitolewa kwa nyakati tofauti na wakazi wa mji wa Mbinga walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, walisema kuwa ni jambo la kushangaza kuona ujenzi wa barabara hiyo baada ya magari kuruhusiwa kupita, hata kabla haijamaliza miezi miwili tabaka la juu la lami limeanza kubomoka.

Saturday, October 4, 2014

SHULE YAKOSA VYOO KAMATI YA UJENZI LAWAMANI

Baadhi ya watoto wa shule ya msingi Mbambi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakiwa kwenye ukumbi wa Umati mjini hapa wakishuhudia kufanyika kwa tendo la mahafali kwa wanafunzi wenzao, ambao wamehitimu darasa la saba. (Picha na Kassian Nyandindi)

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KAMATI ya ujenzi shule ya msingi Mbambi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, imetakiwa kuchukua hatua za haraka juu ya ujenzi wa vyoo katika shule hiyo ili kuwafanya wanafunzi, waweze kuondokana na tatizo la kupanga foleni pale wanapohitaji kujisaidia.

Aidha imeshushiwa lawama kwa kuzembea kutekeleza suala hilo huku ikielezwa kuwa mahitaji ya vyoo katika shule hiyo ni matundu 18 lakini yaliyopo sasa ni nane tu, ambayo hutumia wanafunzi hao na kufanya tatizo hilo kuwa kero miongoni mwao.

Hayo yalisemwa na Gerold Ndunguru alipokuwa mgeni rasmi katika mahafali ya darasa la saba shule ya msingi Mbambi, yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa.

“Ndugu zangu hii ni aibu kwa shule hii ambayo ipo hapa Mbinga mjini kusikia haina vyoo, napenda kusisitiza kamati ya ujenzi ione umuhimu juu ya jambo hili kupewa kipaumbele na namna gani inashirikisha wazazi kwa karibu katika kutatua kero hii”, alisema Ndunguru.

Thursday, October 2, 2014

WAKULIMA WA KAHAWA WAIANGUKIA SERIKALI, WAITAKA KUENDELEA KUIWEZESHA TaCRI

Meneja Kanda ya kusini wa Taasisi ya utafiti wa zao la kahawa kituo cha TaCRI - Ugano kilichopo makao yake makuu wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, Godbless Shao akitoa maelezo mafupi juu ya maendeleo ya zao la kahawa kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) walipokuwa katika kijiji cha Kilimani wilayani humo hivi karibuni.
Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

WAKULIMA wa kahawa wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wameitaka serikali kuendelea kuiwezesha taasisi ya utafiti wa zao hilo hapa nchini (TaCRI) kwa lengo la kuboresha uzalishaji kwa wakulima binafsi na waliopo katika vikundi, ili waweze kuzalisha miche ya kahawa kwa wingi.

Sambamba na hilo pia wameshauri halmshauri za wilaya mkoani humo ambazo hujishughulisha na kilimo cha kahawa, kuongeza maeneo ya uzalishaji kwa kufuata kanuni bora za kilimo, ikiwemo matumizi ya aina mpya ya miche ya kahawa (vikonyo) ambayo haishambuliwi na wadudu waharibifu kwa urahisi.

Rai hiyo ilitolewa na wakulima hao walipokuwa wakizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti, ambao waliwatembelea kuona changamoto wanazokabiliana nazo na faida wanazopata baada ya TaCRI kutoa huduma zake.

Wednesday, October 1, 2014

JENEZA LAIBWA, LAKUTWA KWA AFISA MTENDAJI

Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela

Na Mwandishi wetu,
Songea.
JESHI la Polisi mkoani Ruvuma linawasaka watu wasiofahamika wanaotuhumiwa kuingia msikitini na kuiba jeneza, wilayani Namtumbo, mkoani humo.

Baada ya kuiba jeneza hilo watu hao wanadaiwa kwenda nyumbani kwa Afisa mtendaji wa kijiji cha Kitanda wilayani humo, Fidea Mbawala (30) na kuliweka mlangoni, likiwa limesheheni matofali.

Kamanda wa Polisi mkoa huo Mihayo Msikhela, alisema  tukio hilo lililotokea juzi majira ya asubuhi katika kijiji hicho.

Alisema tukio hilo limesababisha kuwapo utata na kwamba uongozi wa msikiti umedai kuwa tukio hilo ni la aina yake, ambalo halijawahi kutokea.

IDADI YA WALIOKUNYWA TOGWA YENYE SUMU WAONGEZEKA


Na Muhidin Amri,
Songea.


IDADI ya watu walioathirika kutokana na kunywa kinywaji aina ya togwa ambacho kinasadikiwa kuwa na sumu, katika kijiji cha Litapaswi kata ya Mpitimbi wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, imeongezeka kutoka 250 na kufikia watu 325.

Akizungumza na Waandishi wa habari mjini hapa, Kamanda wa Polisi wa mkoa huo Mihayo Msikhela alisema tukio ilo limetokea juzi katika kijiji hicho, wakati watu hao wakiwa kwenye sherehe ya kipaimara ya mwanafunzi wa darasa la sita Dickson Nungu ambaye anasoma  shule ya msingi  Litapwasi.

Kamanda Mihayo alifafanua kuwa kati ya waathirika hao watu 29 wamelazwa katika hospitali ya misheni Peramiho, ambapo kati yao wanaume wapo wane na wanawake 22.

WASHUSHIWA KIPIGO NA KUFARIKI DUNIA



Na Mwandishi wetu,
Ruvuma.

WATU wawili kati ya watatu ambao majina yao hayajafahamika hadi sasa mjini hapa, wanaodaiwa kuwa ni wezi  wamefariki dunia baada ya kushushiwa kipigo na wananchi wenye hasira kali, wakati wakiiba pikipiki.

Wezi hao walikamatwa wakiiba pikipiki tatu zenye namba za usajili T 5888 CJC, T363 BFL na T445 CJT zote aina ya Sanlg.

Katika tukio hilo wezi hao walimjeruhi kwa nondo  Vasco Dagama fundi pikipiki mkazi wa Matogoro Manispaa ya Songea na kumnyanganya pikipiki yenye namba za usajili T363 BFL aina ya Sanlg.

AFARIKI DUNIA BAADA YA KUNYWA DAWA KWA MGANGA WA KIENYEJI



JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI
JESHI LA POLISI TANZANIA



ANUANI YA SIMU:  POLISI RUVUMA   
NAMBARI YA SIMU 025-26 KAMANDA  WA POLISI  025-2602266    MKOA WA RUVUMA
FAX NO. 025-2600380 S.L.P.19,
 SONGEA.


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
MTU MMOJA AMEFARIKI KWA IMANI ZA KISHIRIKINA MKOANI RUVUMA

Mnamo tarehe 22/09/2014 majira ya saa kumi na moja jioni huko mtaa wa Ruvuma manispaa ya Songea Emeresiana Goliama (70), Mngoni, Mkristo na mkazi wa Ngahokola amefariki dunia wakati akipelekwa hospitali ya Mkoa wa Ruvuma kwa matibabu, baada marehemu na wana ukoo wenzake wapatao kumi, kwenda kwa mganga wa kienyeji maarufu kwa jina la Angaza aliyewaambia kuwa kati yao wanne ni wachawi akiwemo marehemu walinyolewa nywele na kunyweshwa dawa kitendo kilicho pelekea hali ya Emeresiana kubadilika ghafla.

Wanaukoo hao walifikia uamuzi wa kwenda kwa mganga baada ya kukaa kikao na kujadili matatizo ya ukoo wao ikiwa ni pamoja na kupata kichaa na ugonjwa wa kifafa, hivyo mganga aliwataja watu wanne kuwa ni wachawi 1. Meresiana Goliama, ambaye ndiye marehemu 2. Oruban Goliama, (75), mkulima, Mkristo, Mngoni na mkazi wa Ngahokola 3. Nikola Huma, (68), mkulima Mristo na mkazi wa Ngahokola 4. Razaria Matembo, (64), Mkristo, Mngoni, mkulima na mkazi wa Ngahokola.

Kufuatia hali hiyo Jeshi la Polisi Mkoa wa Ruvuma linawashikilia watu watatu 1. Daudi Goliama (49), Mngoni, Mkristo na mkazi wa Ngahokola 2, Samson Goliama (40), Mngoni, Mkristo na mkazi wa Ngahokola wote hao wanamuita marehemu shangazi na 3. Rafael Goliama (29), Mngoni, Mkristo na mkulima wa Ngahokola ambaye ni mjukuu wa marehemu, kwa hatua zaidi za kisheria.

Aidha kufuatia hali hiyo wananchi wanatakiwa kutojihusisha na imani za kishirikina ambazo mwisho wake zinapelekea kupoteza maisha na chuki kwa jamii.    

Sunday, September 21, 2014

CHUO KIKUU CHA SAYANSI SONGEA CHA PONGEZWA KWA JITIHADA ZAKE


Na Mwandishi wetu,

Songea.

MKUU wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu amekipongeza chuo kikuu cha sayansi ya kompyuta cha Mtakatifu Joseph tawi la Songea mkoani humo, kwa jitihada zake za kuendelea kupanua wigo wa kutoa huduma na kukuza elimu ya juu hapa nchini.

Mwambungu alitoa pongezi hizo alipokuwa akihutubia kwenye mahafali ya tano ya chuo hicho mjini hapa, kwa wahitimu 119 wa shahada na stashahada ambapo alisema kuwa kuanzishwa kwa chuo hicho, kumesaidia kulipunguzia taifa tatizo la ukosefu wa wataalam wa sayansi hususan katika ukanda wa kusini na taifa kwa ujumla.

Alisema kuwa kuanzishwa kwa chuo kikuu cha sayansi ya kilimo na teknolojia katika sekta ya kilimo, ni jambo jema kwa ustawi wa nchi na uti wa mgongo na mwajiri mkubwa kwa wananchi huku akiwataka wahitimu hao kutumia elimu waliyoipata kwa ajili ya kuleta mabadiliko chanya katika jamii.

Alieleza kuwa katika maisha ya sasa hakuna njia fupi ya kufikia mafanikio katika maisha  zaidi ya kufanya kazi kwa bidii na maarifa, na kwamba changamoto zilizopo katika chuo hicho zigeuzwe kuwa fursa pekee ya kujipanua na kutoa elimu bora,  huku akiwataka kuboresha mawasiliano ili kukuza wigo wa utatuzi wa changamoto hizo.

Friday, September 19, 2014

MKUU WA MKOA RUVUMA AKUTANA NA MADEREVA PIKIPIKI, ASISITIZA AMANI NA UTULIVU


Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu, akizungumza na waendesha pikipiki (Maarufu kama  Boda Boda) leo katika ukumbi wa Songea Club uliopo Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma. Mwambungu amewataka madereva Boda boda kuepusha ajali za barabarani kwa kufuata sheria, na kutotumiwa na vyama vya kisiasa.

Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

BAADA ya siku chache kupita kufuatia tukio la nani amefanya kitendo kiovu cha kurusha bomu la kienyeji katika mtaa wa Msufini Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, na kujeruhi baadhi ya askari Polisi mjini hapa, Mkuu wa mkoa huo Said Mwambungu amekutana na waendesha pikipiki wa manispaa hiyo na kuwataka  kujenga ushirikiano ili kuweza kulinda amani ya nchi dhidi ya maadui ambao hawalitakii mema taifa hili.

Mwambungu amekutana leo na madereva hao maarufu kwa jina la “Boda boda” katika ukumbi wa Songea Club uliopo mjini Songea, akisisitiza kujenga ushirikiano kwa vyombo vya usalama ili kuweza kupata ukweli wa tukio hilo na kuwafanya wakazi wa mji huo, watu wengine (wageni) wanaoingia na kutoka kuondoa hofu na kuishi katika hali ya usalama.

Akizungumza kwa njia ya simu na mwandishi wa habari hizi, Mkuu huyo wa mkoa alisisitiza kuwa jamii ihakikishe kwamba amani utulivu vinatawala miongoni mwao, na pale wanapoona kuna sintofahamu ni vyema watoe taarifa katika vyombo husika vya usalama ili kuweza kubaini uhalifu unaofanyika na hatua ziweze kuchukuliwa haraka dhidi ya wahalifu.

JESHI LA POLISI NCHINI LANYOSHEWA KIDOLE LATAKIWA KUACHA KUNYANYASA WAANDISHI WA HABARI

Rais Jakaya Kikwete wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

















Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

JESHI la Polisi nchini limetakiwa kuacha vitendo vya  kuwanyanyasa waandishi wa habari na kuwafanya wasitekeleze wajibu wao ipasavyo, kufanya hivyo ni kutowatendea haki na kudhalilisha taaluma ya habari.

Sambamba na hilo Jeshi hilo limenyoshewa kidole kwamba limekuwa na historia ya kupiga na kuwafukuza waandishi wa habari, hasa pale wanapotafuta ukweli juu ya matukio mbalimbali ambayo yamekuwa yakitokea miongoni mwa jamii.

Rai hiyo imetolewa na baadhi ya Wananchi wa mkoa wa Ruvuma, walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti kufuatia tukio lililotokea jana makao makuu ya jeshi hilo baada ya waandishi kupigwa, kukimbizwa na mbwa ili wasichukue taarifa za kuhojiwa kwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Freeman Mbowe.

Thursday, September 18, 2014

JESHI LA POLISI NCHINI LATHIBITISHA BOMU WALILORUSHIWA ASKARI WAKE MJINI SONGEA LIMETENGENEZWA KIENYEJI

 Eneo la tukio mtaa wa Msufini mjini Songea mkoani Ruvuma, ambako bomu ambalo limetengenezwa kienyeji lilirushwa kwa mkono na watu wasiojulikana Jeshi la Polisi likiwa limezungushia alama.
Askari Ramadhani Ally, akiwa amelazwa katika hospitali ya mkoa wa Ruvuma iliyopo mjini Songea, akielezea kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) jinsi mkasa huo ulivyowakuta na askari wenzake wakati walipokuwa doria mtaa wa Msufini mjini hapa,  baada ya kurushiwa bomu ambalo limetengenezwa kienyeji na watu wasiojulikana mpaka sasa.

Na Kassian Nyandindi,
Songea.


JESHI la polisi nchini limethibitisha kuwa kitu kilichokuwa kinadaiwa kuwa ni bomu lililorushwa mjini Songea mkoani Ruvuma, na kuwajeruhi askari wa jeshi hilo mjini hapa kuwa ni la kutupwa kwa mkono.

Tukio hilo lilitokea  Septemba 16 mwaka huu majira ya saa 1.25 usiku katika eneo la Misufini na kuwajeruhi askari polisi watatu kati ya wanne waliokuwa doria na kwamba bomu hilo limetengenezwa kienyeji.

Akitoa taarifa ya uchunguzi wa tukio hilo kwa waandishi wa habari mjini hapa, Mkurugenzi wa upelelezi wa makosa ya jinai kamishina wa polisi Isaya Mngulu amesema bomu hilo lilirushwa na watu wasiojulikana na kuwajeruhi askari polisi watatu waliokuwa doria siku hiyo.

Mngulu alisema askari hao ni wa kituo kikuu cha polisi mjini Songea ambao aliwataja kuwa ni G.5515 PC John, G7351 PC Ramadhan na WP 10399 Felista ambapo baaada ya kujeruhiwa kwa bomu hilo, walikimbizwa katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Ruvuma kwa ajili ya matibabu.

KATIBU TAWALA MSAIDIZI MKOANI RUVUMA NA WENZAKE WAPANDISHWA KIZIMBANI KWA WIZI WA SHILINGI MILIONI 800

Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MWENYEKITI wa chama kikuu cha ushirika (SONAMCU) wilaya Namtumbo mkoani Ruvuma, amefikishwa katika Mahakama ya mkoa huo akiwemo na Katibu tawala msaidizi wa mkoa huo ambaye pia ni afisa ushirika wa mkoa huo, kwa tuhuma za kula njama, kugushi nyaraka na kuiba fedha shilingi milioni 889.

Imedaiwa mahakamani hapo na mwanasheria wa serikali Hamimu Mkoleye mbele ya Hakimu mkazi mfawidhi wa Mahakama ya mkoa huo Joackimu Tiganga washtakiwa hao wote wawili wanalinganishwa na washitakiwa wengine 14 ambao walikwisha somewa mashitaka na kufanya idadi yao kuwa 16 ambapo wanadaiwa kuiba fedha hizo.

Mkoleye amewataja waliofikishwa mahakamani hapo kuwa ni Ally Athumani Bango (45) Mwenyekiti wa chama kikuu cha ushirika Namtumbo (SONAMCO) ambacho kinajishughulisha na ununuzi wa zao la tumbaku.

AHUKUMIWA KWENDA JELA BAADA YA KULAWITI



Na Mwandishi wetu,
Songea.

MKAZI mmoja wa Mjimwema Songea mjini mkoani Ruvuma, amehukumiwa na Mahakama ya Hakimu mkazi wa mkoa huo adhabu ya kifungo cha maisha  kwenda gerezani kwa kosa la kumlawiti msichana mwenye umri wa miaka tisa.

Akisoma hukumu hiyo hakimu mkazi mfawidhi wa mkoa huo, Joakimu Tiganga alisema kuwa mahakama imeridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka kuwa John Mapunda (38) mkazi wa Mjimwema songea mjini bila halali alimlawiti msichana huyo.

DEREVA PIKIPIKI AKUTWA AMEFARIKI DUNIA BAADA KUCHOMWA KISU TUMBONI



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MTU mmoja ambaye ni dereva wa pikipiki amekutwa amefariki dunia baada kuchomwa kisu tumboni na kupigwa na kitu kizito kichwani kisha mwili wake kufungwa kamba mikononi na miguuni hatimaye kuunganishwa kwenye mti na watu wasiojulikana.

Tukio hilo lilitokea Septemba 16 mwaka huu majira ya mchana ambapo mwili wa marehemu huyo umetambuliwa kwa jina la Maulid Kuburi (21) mkazi wa kijiji cha Mpandangindo Songea vijijini mkoani Ruvuma.

Mwili wa marehemu huyo umekutwa na majeraha ambapo alichomwa kisu mara tatu tumboni kisha kufariki dunia.

ASKARI SONGEA WAJERUHIWA NA KITU KINACHODAIWA KUWA NI BOMU LA KURUSHWA NA MKONO



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

ASKARI watatu  wa Jeshi la Polisi mkoani Ruvuma, wamelazwa katika hospitali ya mkoa huo iliyopo Songea mjini  wakiwa wanapatiwa matibabu baada ya kushambuliwa na kitu kinachodaiwa kuwa ni bomu la kurusha kwa mkono.

Tukio hilo limetokea Septemba 16 mwaka huu majira ya jioni katika kata ya Msufini mjini hapa, ambapo wamejeruhiwa.

Akizungumzia tukio hilo kaimu kamanda wa polisi wa mkoa huo ASP George Chiposi,  alisema kuwa watu watatu wasio fahamika ndio waliotupa kitu hicho kinacho sadikiwa kuwa ni bomu la kutupwa kwa mkono.

Bomu hilo alisema limetengenezwa kienyeji na kuwajeruhi askari  hao watatu waliokuwa doria.

Wednesday, September 10, 2014

SERIKALI YARUHUSU WAFANYABIASHARA KUUZA MAHINDI NJE YA NCHI



Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

SERIKALI hapa nchini imeruhusu wafanyabiashara kuuza mahindi yao nje ya nchi popote pale, huku ikiwataka kuzingatia bei elekezi iliyowekwa ili kumfanya mkulima asiweze kupata hasara.

Sambamba na hilo mahindi ambayo yamehifadhiwa katika vituo husika vilivyopo mkoani humo, serikali itayanunua kwa kilo shilingi 500 na kwamba wakulima hawaruhusiwi kuingiza mahindi mengine katika vituo.

BASI LA SUPER FEO LAPATA AJALI LEO WATATU WAFARIKI DUNIA 25 WAJERUHIWA VIBAYA



 



Picha hizi zinaonesha basi lenye namba za usajili T 273 CDD mali ya kampuni ya Super Feo lililopata ajali katika kijiji cha Sanangula mkoani Ruvuma, ambalo lilikuwa likisafiri leo kutoka Songea mjini kwenda mkoani Mbeya.
 


Na Kassian Nyandindi,

Songea.

WATU watatu wamefariki dunia na wengine 25 wamejeruhiwa vibaya baada ya basi walilokuwa wakisafiria kutoka Songea mjini mkoani Ruvuma, kwenda  jijini Mbeya kumgonga mwendesha baiskeli na baadaye kupinduka.

Habari zilizopatikana leo mjini hapa ambazo zimethibitishwa na Kamanda wa polisi mkoani Ruvuma, Mihayo Msikhela amesema kuwa tukio hilo limetokea majira ya saa 4:45 asubuhi, katika eneo la Sanangula nje kidogo ya Manispaa ya songea mkoani humo.

Kamanda Msikhela amefafanua kuwa ajali hiyo imetokea kwenye barabara ya kutoka Songea kwenda Njombe, ambapo namba za gari yenye usajili T273 CDD aina ya Mitsubishi Rosa mali ya kampuni ya Super feo mjini Songea ambalo lilikuwa linatoka Songea kwenda Mbeya.

Tuesday, September 9, 2014

MKUU WA WILAYA MBINGA AWA MBOGO, AWASHUKIA WAFANYABIASHARA WA KAHAWA



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga amewashukia wafanyabishara wenye tabia ya kutorosha kahawa wilayani humo kwa lengo la kukwepa kulipa ushuru na kuwataka kuacha tabia hiyo mara moja, na atakaye endelea kufanya hivyo pale atakapobainika atachukuliwa hatua kali za kisheria ikiwemo kunyang’anywa kibali cha ununuzi wa zao hilo wilayani humo.

Alitoa onyo hilo wakati alipokuwa akifunga kikao cha wadau wa kahawa kanda ya Ruvuma, kilichofanyika katika ukumbi wa Jimbo Katoliki mjini hapa.

WATAKIWA KUZALISHA MICHE YA KAHAWA KWA WINGI



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MKURUGENZI mkuu wa bodi ya kahawa Tanzania (TCB) Adolf  Kumburu ameziasa Halmashauri na taasisi mbalimbali hapa nchini ambako zao la kahawa linazalishwa, kuhakikisha kwamba wanashiriki kikamilifu katika kuzalisha miche bora ya kahawa ili kuweza kuwafikia wakulima walio wengi kiurahisi na kukua kwa uzalishaji wa zao hilo.

Alisema pamoja na Taasisi ya utafiti wa kahawa nchini (TaCRI) kuzalisha miche hiyo na kuisambaza, bado haitoshelezi mahitaji, kutokana na uzalishaji kuwa mdogo hivyo ili kuondokana na tatizo hilo wakulima, halmashauri na taasisi zingine zinapaswa kushiriki katika kuanzisha bustani mama za kuzalishia miche ya kahawa.