Friday, December 16, 2016

AGIZO LA WAZIRI KUWASIMAMISHA KAZI WATENDAJI TASAF MBINGA LATEKELEZWA

Na Kassian Nyandindi,         
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Cosmas Nshenye amesema kwamba amesikitishwa na kitendo cha maofisa Washauri na Wafuatiliaji Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) wilayani humo ambao walipewa dhamana ya kusimamia zoezi la ugawaji wa fedha kwa kaya maskini, kutotekeleza majukumu yao ipasavyo na kusababisha fedha hizo kulipwa watu ambao hawakuwa na sifa.  

Cosmas Nshenye.
Aidha alifafanua kuwa kufuatia hali hiyo serikali wilayani hapa imechukua hatua ya kumsimamisha kazi Mratibu wa mfuko huo, Ahsante Luambano ambaye alisema kuwa ameshindwa kuwajibika kwa kusimamia ipasavyo zoezi la uibuaji wa kaya hizo na kusababisha wengi wao walioingizwa katika mpango wa kulipwa fedha hizo kuwa ni viongozi wa serikali ngazi ya vijiji na vitongoji.

Mkuu huyo wa wilaya ya Mbinga, Nshenye alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, huku akiongeza kuwa barua ya Waziri mwenye dhamana ya Desemba 5 mwaka huu ambayo waliipata imetoa maagizo ya kuwasimamisha kazi waliohusika katika kuvuruga utekelezaji wa mpango huo kwa muda usiojulikana hadi uchunguzi utakapokamilika na wahusika kuchukuliwa hatua za kinidhamu.


Nshenye alisema kuwa licha ya kusimamishwa kazi mratibu huyo, pia hatua za kuwasimamisha watendaji wengine walioshiriki kuhujumu fedha za mfuko wa TASAF wilayani Mbinga zinafuata na taarifa ya idadi yao kuwa ni wangapi itatolewa baadaye lengo ikiwa waweze kupisha uchunguzi kufanyika kuhusiana na jinsi walivyojihusisha kuvuruga utekelezaji wa mfuko huo.

“Kwa mujibu wa utafiti ambao unaendelea kufanyika, hivi sasa ninataarifa kwamba zaidi ya walengwa hewa 200 waliandikishwa kwenye mpango huu wa kupewa fedha hapa Mbinga, wengi wao tuna taarifa kwamba ni viongozi wa serikali ngazi ya vijiji kwa kweli haingii akilini kwa kiongozi wa serikali kuingizwa kwenye mpango wa kaya maskini wakati anao uwezo wa kumudu maisha yake”, alisema Nshenye.

Alieleza kuwa endapo watabainika kwa namna moja au nyingine baada ya uchunguzi unaoendelea kufanyika kwamba wamehusika kuyafanya hayo watachukuliwa hatua kali za kinidhamu ikiwemo kufukuzwa kazi ili iwe fundisho kwa wengine na jambo hilo lisiweze kujirudia tena.

Hata hivyo Mkuu huyo wa wilaya ya Mbinga alisisitiza kuwa utafiti unaoendelea kufanyika unatekelezwa kwa kupita kaya kwa kaya, ili waweze kujiridhisha wanufaika hewa jumla yake ni wa ngapi na nani alistahili kupewa fedha hizo za TASAF.

No comments: