Wednesday, December 14, 2016

WANANCHI MBINGA KUENDELEA KUNUFAIKA NA MPANGO WA UPIMAJI ARDHI


Mkurugenzi mtendaji Halmashauri wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Gombo Samandito akizungumza na wakazi wa tarafa ya Mbuji juzi kuhusiana na mpango wa halmashauri hiyo kuanza mchakato wa kuanzishwa kwa miji midogo sambamba na  uendelezaji wa miji hiyo, ambapo baadhi ya maeneo yatachukuliwa na serikali kwa ajili ya kupisha huduma mbalimbali za kijamii kama vile ujenzi wa shule, zahanati, miundo mbinu ya maji na barabara.

Na Kassian Nyandindi,         
Mbinga.

HALMASHAURI ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, imejiwekea mkakati wa kupanga na kupima maeneo yote ya bonde la Hagati na tarafa ya Mbuji yaliyopo wilayani humo, kutokana na wakazi wanaoishi katika maeneo hayo kuendeleza maeneo yao kwa kujenga makazi holela.

Aidha imeelezwa kuwa sababu nyingine inayoifanya halmashauri hiyo kutaka kutekeleza mpango huo ni ongezeko kubwa la idadi ya watu wanaoishi katika maeneo hayo, huku ardhi iliyopo haitoshelezi kwa matumizi ya binadamu na asilimia kubwa wananchi wake wamekuwa wakitumia maeneo yao kwa shughuli za kilimo cha zao la kahawa.

Vilevile imefafanuliwa kuwa maeneo ya bonde hilo la Hagati na tarafa ya Mbuji hayana mgawanyiko rasmi wa matumizi ya ardhi hivyo halmashauri hiyo ya wilaya ya Mbinga, inakusudia kupanga na kupima maeneo ya wananchi bila kuathiri hali halisi ya mazingira yaliyopo sasa kwa kuzingatia kanuni na taratibu za sheria ya ardhi namba 4 ya mwaka 1999 pamoja na sheria ya mipango miji namba 7 ya mwaka 2007.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Gombo Samandito alisema hayo juzi alipokuwa akitoa elimu kwa wananchi juu ya mapendekezo ya upangaji ardhi katika maeneo hayo, kwa lengo la kuondoa ugumu wa kusambaza huduma za kijamii kwa wananchi hao kama vile huduma ya ujenzi wa miundombinu ya barabara, maji, zahanati na shule ili kuweza kumfikia kila mwananchi katika eneo husika.

Samandito alisema kuwa eneo kubwa la bonde la Hagati na tarafa ya Mbuji limekuwa likitumika kwa shughuli hizo za kilimo na kusababisha upungufu mkubwa wa maeneo ya matumizi mengine ya huduma za kijamii kama vile ujenzi wa masoko, viwanda vidogo vidogo, maeneo ya wazi na yale ya kufanyia biashara.

“Kukua na kuongezeka kwa uhitaji wa makazi ya wananchi katika maeneo haya pamoja na eneo kubwa la ardhi kupandwa zao la kudumu la kahawa kumepelekea tuwe na ongezeko kubwa la ujenzi usio rasmi, yaani makazi holela ambayo kwa namna moja au nyingine yameongeza kasi ya matumizi ya ardhi hivyo ni lazima tupange miji yetu kwa utaratibu unaotakiwa ili tuweze kunusuru hali hii kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye’, alisisitiza Samandito.

Mkurugenzi huyo aliongeza kuwa upimaji huo wa ardhi utakapokamilika mwananchi anayemiliki kipande chake cha ardhi baada ya kupimwa, atapewa hati miliki huku akifafanua kuwa ekari moja itakuwa ikipimwa kwa gharama ya shilingi 100,000 ambayo mwananchi huyo atapaswa kulipia.

Kwa upande wao wananchi wanaoishi katika maeneo ya bonde la Hagati na tarafa ya Mbuji wilayani hapa, waliupokea mpango huo kwa mikono miwili huku wakisema kwa nyakati tofauti kuwa hawawezi kuukataa kwani ni jambo muhimu kwa maendeleo yao na taifa kwa ujumla.

Hata hivyo walisema kuwa upimaji huo utaweza kusaidia pia kuzuia kuzuka kwa migogoro ya ardhi kiholela, ambayo inasababishwa na tatizo la kutokuwepo kwa mipaka inayotambulika kisheria na kuikosesha pia serikali mapato yake yanayotokana na kodi ya ardhi ambayo mara nyingi hutolewa kwa uthaminishaji wa maeneo yaliyopimwa.

No comments: