Wednesday, December 7, 2016

NAMTUMBO WAANZA MCHAKATO WA KUANZISHA KITUO CHA KURUSHA MATANGAZO

Na Kassian Nyandindi,         
Namtumbo.

HALMASHAURI ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, imeanza mchakato wake wa kuanzisha kituo cha kurusha matangazo (Redio ya jamii) ambayo itakuwa ikiyarusha ndani ya wilaya hiyo, kwa lengo la kuhamasisha maendeleo mbalimbali ya wananchi.

Yeremias Ngerangera ambaye ni Ofisa habari wa wilaya hiyo aliwaeleza waandishi wa habari kuwa mchakato wa kuanzisha Redio hiyo ya jamii, unaendelea vizuri ambapo tayari kamati ya kusimamia suala hilo imeundwa na kuanza kazi yake.

Alitaja idara zilizopo kwenye kamati hiyo ni idara ya mipango, utawala, maendeleo ya jamii, afya, mazingira pamoja na kitengo cha sheria na usalama ambazo zinatoka katika halmashauri ya wilaya ya Namtumbo.


Kadhalika alibainisha kuwa sababu za halmashauri hiyo kuanzisha kituo hicho cha kurusha matangazo ni pamoja na kurahisisha mawasiliano kati ya uongozi wa halmashauri, wananchi na wilaya kwa ujumla juu ya maagizo mbalimbali ambayo yanatolewa kwa kuwataka wananchi wake waweze kuyatekeleza.

Pia Redio hiyo itatumika kuelimisha jamii juu ya masuala ya kuzingatia kilimo bora, umuhimu wa utunzaji wa mazingira, kuhamasisha kupeleka watoto shule, kuwa na afya bora na mambo mengine ya kimaendeleo.

Naye Kaimu Ofisa mipango wa halmashauri ya wilaya hiyo, Gwakisa Mwaseba ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya kusimamia mchakato wa kuanzisha Redio hiyo, alisema kuwa zaidi ya shilingi milioni 103,400,000 zinahitajika ili kuweza kukamilisha zoezi hilo.

Gwakisa aliongeza kwa kuwataka wadau kutoka sehemu mbalimbali ndani na nje ya Namtumbo, kushirikiana kwa pamoja katika kuchangia uanzishaji wake pamoja na maendeleo ya wilaya kwa ujumla.

Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Christopher Kilungu ameitaka kamati hiyo iliyoundwa kusimamia kikamilifu zoezi hilo kwa kufanya utekelezaji husika kwa weledi na kuhakikisha unaleta ufanisi mkubwa, ili wananchi wa Namtumbo waweze kuwa na Redio yao ya kijamii.


Vilevile wananchi wa wilaya hiyo walipoelezwa kupitia mikutano ya hadhara juu ya kuanzishwa kwa kituo hicho cha kurusha matangazo, walifurahishwa na hatua hiyo huku wakisema ni nzuri yenye kuwafanya waweze kusonga mbele kimaendeleo.

No comments: