Saturday, December 24, 2016

WAGANGA WAKUU WA MIKOA NA WILAYA KIKAANGONI WAZIRI ASHANGAZWA KUPATA TAARIFA HOSPITALI HAZINA DAWA

Na Kassian Nyandindi,          
Mbinga.

NAIBU Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Suleiman Jaffo amesema kuwa ameshangazwa kupata taarifa kwamba baadhi ya hospitali za serikali hapa nchini hazina dawa, wakati serikali imekuwa ikituma fedha kila mwezi kwa ajili ya kununua vifaa tiba na madawa ya kutibu wagonjwa.

Suleiman Jaffo.
Aidha kufuatia hali hiyo ametoa onyo kali kwa Waganga wakuu wa mikoa na wilaya kwamba endapo atasikia au kupata taarifa kuwa hospitali hizo hazina madawa, wajiandae kuwajibishwa na kutolea maelezo fedha hizo za kununulia dawa baada ya kuzipokea wamezitumia kwa shughuli gani.

“Sitegemei kusikia hata dawa aina ya Panadol hakuna, serikali imekuwa ikileta fedha kwenye mahospitali yetu kupitia mfuko wa Busket fund lakini taarifa nilizonazo kumekuwa na mchezo mchafu wa kutumia fedha za mfuko huu, watu kulipana posho wakati wananchi wanateseka”, alisema Jaffo.


Hayo yalisemwa na Waziri huyo jana alipokuwa katika ziara yake ya kikazi akizungumza na watumishi wa halmashauri ya mji wa Mbinga na wilaya ya Mbinga vijijini mkoani Ruvuma, kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa.

Jaffo alifafanua kuwa hategemei kusikia mchezo huo wa kuchezea fedha za mfuko huo kwa matumizi ambayo hayaendani na maelekezo husika yaliyotolewa na serikali, hivyo amewaagiza Wakurugenzi wa halmashauri hapa nchini wahakikishe wanasimamia ipasavyo matumizi ya fedha hizo na wananchi waweze kupata dawa pale wanapokwenda kutibiwa katika hospitali za serikali.    

Pamoja na mambo mengine aliongeza kuwa kila baada ya miezi mitatu hospitali ya mji wa Mbinga imekuwa ikipokea zaidi ya shilingi milioni 100 kwa ajili ya kununulia dawa na kwamba kwa upande wa hospitali ya wilaya ya Mbinga, nayo imekuwa ikipokea shilingi milioni 254 kwa ajili ya kununua dawa hizo za kutibu wagonjwa kutoka katika mfuko huo wa Busket fund.


No comments: