Sunday, December 18, 2016

NOVATUS LUAMBANO ANATAFUTWA NA JESHI LA POLISI



Na Gideon Mwakanosya,         
Songea.

Jeshi la Polisi mkoani Ruvuma linamsaka Novatus Luambano (32) mkazi wa kijiji cha Mahanje Madaba wilayani songea, ambaye ni dereva  wa basi dogo ambalo liliacha njia kisha kupinduka na kusababisha kifo cha abiria mmoja na wengine  27 kujeruhiwa vibaya.

Zubery Mwombeji Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma.
Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Zubery Mwombeji amewaambia waandishi wa habari kuwa tukio hilo lilitokea Disemba 15 mwaka huu, majira ya mchana huko katika kijiji cha Hanga Ngadinda wilaya ya Songea vijijini ambapo gari lenye namba za usajili T 435 BHT aina ya Toyota Coster, lililokuwa likiendeshwa na Novatus lilipinduka kutokana na kuwa katika mwendo kasi kisha dereva huyo kutokomea kusikojulikana.

Alimtaja aliyefariki dunia papo hapo katika ajali hiyo kuwa ni Witness Tembe (11) ambaye ni mwanafunzi wa shule ya msingi Matarawe iliyopo katika Manispaa ya Songea mkoani hapa.


Katika ajali hiyo alieleza kuwa watu 27 walijeruhiwa vibaya ambapo kati yao 17 walitibiwa na kuruhusiwa kurudi majumbani kwao na wengine hali zao ni mbaya bado wamelazwa katika hospitali ya mkoa wa Ruvuma kwa matibabu zaidi.

Aliwataja waliolazwa kuwa ni Emilia Haule (21) mkazi wa Njombe mjini, Madia Ally (1), Sailisi Ndunguru (29) na Viligilia Mkinga (52) wote wakazi wa Mjimwema Manispaa ya Songea, Sheiba Hussein (28), Michael Ndunguru (31) na Rajabu Athuman (40) wote wakazi wa kijiji cha Likarangilo nje kidogo ya Manispaa hiyo na kwamba Alatanga Mdowe (45) mkazi wa mji mdogo wa Madaba, Beatrice Nchimbi (29)  mkazi wa Mahanje huku majeruhi mmoja ambaye ni wa jinsia ya kiume hakuweza kutambulika majina yake kutokana na hali yake kuwa mbaya akishindwa kuzungumza.

No comments: