Tuesday, December 20, 2016

HALMASHAURI MANISPAA YA SONGEA KUTUMIA MILIONI 488 UJENZI MRADI WA MAJI RUHUWIKO KANISANI



Na Kassian Nyandindi,            
Songea.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, inatarajia kutumia shilingi milioni 488 kwa ajili ya ujenzi wa mradi wa maji katika mtaa wa Ruhuwiko Kanisani, kwa lengo la kuwaondolea kero upatikanaji wa maji wakazi wanaoishi katika mtaa huo.

Aidha tayari Manispaa hiyo imeingia mkataba na kampuni ya Giraf Investment na kwamba hadi sasa mradi huo, ambao umefadhiliwa na benki ya dunia ujenzi wake umefikia asilimia 95. 

Albano Midelo ambaye ni Ofisa habari wa Manispaa hiyo alisema hayo alipokuwa akihojiwa na waandishi wa habari mjini hapa, huku akiongeza kuwa ni asilimia ndogo imebakia katika kukamilisha ujenzi wake ili wananchi hao waweze kukabidhiwa mradi na kuanza kuutumia.


“Idara ya maji tayari imefanya mkutano wa hadhara na wakazi wa mtaa huu juu ya taratibu za watumiaji maji na namna ya kuchangia, ili mradi uweze kuwa endelevu”, alisema Midelo. 

Midelo alisema kuwa mradi pia unatumia nguvu ya umeme kupandisha maji kwenye tanki kubwa hivyo watumiaji wa maji wanatakiwa kuchangia gharama kidogo kila mwishoni mwa mwezi na kwamba, lengo la idara hiyo katika Manispaa ya Songea ni kuukabidhi mradi katika Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa mazingira (SOUWASA) ambao watasimamia uendeshaji wake.

Wakati huo huo idara hiyo ya maji katika Manispaa hiyo imekamilisha ukarabati wa visima viwili ambavyo vinatarajia kuhudumia watu zaidi ya 500 vilivyopo katika shule ya sekondari Mdandamo, iliyopo kata ya Mletele ambacho kimegharimu shilingi milioni 2.2 na kingine kilichopo shule ya msingi Luhira katika kata ya Mshangano kilichogharimu shilingi milioni 2.8.

No comments: