Wednesday, December 7, 2016

DOKTA KALEMANI AZITAKA TAASISI ZA KIFEDHA KUSHIRIKIANA NA WAWEKEZAJI BINAFSI WANAOZALISHA UMEME

Na Kassian Nyandindi,                
Mbinga.

NAIBU Waziri wa Nishati na Madini Dkt. Medard Kalemani amezitaka taasisi za kifedha hapa nchini kushirikiana na wawekezaji binafsi ambao wanazalisha umeme wa nguvu ya maji, katika kuwapatia mikopo yenye riba nafuu ili waweze kuendesha shughuli ya uzalishaji wa nishati hiyo kwa ufanisi zaidi.

Dkt. Medard Kalemani.
Aidha ameeleza kuwa serikali kwa kushirikiana pia na Wakala wa umeme vijijini (REA) wameweka mikakati ya kuhakikisha kwamba umeme utapelekwa katika maeneo yote ya vijijini na kwenye taasisi za serikali, kwa lengo la kumaliza tatizo la upatikanaji wa huduma hiyo katika maeneo ambayo hayajafikiwa na umeme.

Hayo yalisemwa na Dkt. Kalemani juzi alipokuwa katika ziara yake ya kikazi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakati alipotembelea kituo cha kuzalisha umeme wa nguvu ya maji unaoendeshwa na kampuni ya Andoya Hydro Electric Power(AHEPO) katika kata ya Mbangamao wilayani humo.


“Watanzania wengine waige mfano kama huu, ninawasifu sana mmeweza kuzalisha umeme huu wa nguvu ya maji megawati 500 na kuweza kuunganisha na mini gridi ya TANESCO hapa Mbinga pamoja na kuwasambazia wananchi vijiji jirani ambao sasa wanautumia kwa shughuli zao mbalimbali za kimaendeleo”, alisema Dkt. Kalemani.

Awali akitolea maelezo juu ya maendeleo ya mradi huo, Jasper Bubelwa ambaye ni Injinia mkuu wa mradi wa AHEPO alimweleza Dkt. Kalemani kuwa hivi sasa kampuni hiyo, inashindwa kufikia malengo husika ya kuendelea kujenga njia za kusafirisha umeme katika maeneo ya baadhi ya vijiji kutokana na mabenki ya biashara na taasisi za kifedha kutoza riba kubwa.

Injinia Bubelwa alieleza kuwa pia wanafanya jitihada ya kutafuta fedha kwa ajili ya kuongeza mashine ya pili yenye uwezo wa kuzalisha megawati 500 za umeme ili waweze kufikia malengo ya kukamilisha uzalishaji wa megawati 1 na kuweza kuendelea kuwasambazia wananchi.

Hata hivyo hadi kukamilika kwa ujenzi wa miundombinu ya mradi huo na kusambaza nishati hiyo, jumla ya wateja 922 wanatarajiwa kufikiwa kati ya 3,835 waliopo katika vijiji vya Lifakara, Kilimani na Mbangamao na ziada ya nishati ya umeme kuunganishwa kwenye mfumo wa mini gridi ya Shirika la Umeme Tanzania iliyopo hapa wilayani Mbinga.


No comments: