 |
Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. |
Na Kassian Nyandindi,
SIKU zote misingi ya taifa linalojali maisha ya wananchi wake
ni ujenzi bora wa elimu, afya na miundombinu inayokuza uchumi huku viongozi
wake katika eneo husika hutakiwa kuwa makini, kujenga mshikamano na kuacha
migogoro ya hapa na pale.
Wahenga wetu husema, ukiona kiongozi muda mwingi amekuwa
akiendekeza migogoro basi tambua kwamba, mahali pale ameshindwa kutawala na
maendeleo hayawezi kupatikana badala yake serikali, inashauriwa kuchukua hatua
za haraka katika kunusuru hali hiyo ili wananchi wake wasipate mateso.
Kinyume chake kukosekana kwa kiongozi wa kweli na asiyejali
utawala bora au maslahi ya wananchi, kunanyima watu fursa ya kufanya maamuzi sahihi
kuhusu rasilimali zao, ikiwemo hata kujiondoa katika lindi la umasikini
unaonuka.
Popote pale kiongozi wa namna hii, ni sawa na kusema ni kiongozi
muflisi ambaye hutambulika muda mwingi kupenda kuruhusu mianya ya rushwa
kutawala kila kona, hasa wakati wa utoaji wa huduma muhimu kwa wananchi anaowaongoza.
Katika makala haya napenda kuelezea juu ya kilio cha baadhi
ya wananchi wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, dhidi ya Mkuu wao wa wilaya Senyi
Ngaga na Mkurugenzi wake Hussein Ngaga, jinsi gani wanavyoiyumbisha wilaya hiyo
na kufikia hatua wananchi kukosa imani nao.
Nimefikia hatua ya kuliweka jambo hili hadharani kutokana na
mambo kadhaa yanayokera wananchi ambayo viongozi hawa, wamefikia sasa kuchukiwa
na watu wanaowaongoza kutokana na kile kinachoelezwa kuwa kupenda kufanya mambo
ambayo hayana msingi katika mustakabali mzima, wa maendeleo ya wananchi wa
wilaya hiyo.
Jambo la kwanza, kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali ambavyo
vimetoa ushirikiano wa karibu kwa mwandishi wa makala haya, vimeeleza kuwa mkuu
wa wilaya hiyo ameshindwa kukemea mgogoro ambao unaendelea kufukuta kwa muda
mrefu kati ya mkurugenzi huyo na afisa elimu msingi wa wilaya hiyo, Mathias
Mkali.
Aidha wanaongeza kuwa licha ya afisa elimu huyo kuonekana
kufanya kazi zake vizuri katika kuboresha kiwango cha taaluma wilayani humo,
cha kushangaza viongozi hao wamekuwa wakimpiga vita pasipo sababu yoyote ya
msingi na kusababisha kuwepo kwa tabaka kubwa, ambalo linaitafuna wilaya kwa
kurudisha nyuma maendeleo katika sekta hiyo muhimu.
Wanasema mkuu wa wilaya Ngaga, kukaa kwake kimya pamoja na serikali
kukemea migogoro kazini huenda akawa amejenga maslahi yake binafsi, na kusahau
jukumu alilopewa na Rais Jakaya Kikwete, wakati anamteua kwenda kutumikia
wananchi wa wilaya hiyo kwa kuzingatia kuepuka misingi ya itikadi, rangi au
dini na mambo mengine ambayo hayana tija katika jamii.
Wengi kwa nyakati tofauti wanasema, vitendo vinavyofanywa na
mkurugenzi huyu huku mkuu huyo wa wilaya kutoingilia kati na kukemea, ni sawa
na kushughulika kukomoa wananchi badala ya kubuni na kusimamia maendeleo kwa
faida ya kizazi cha sasa na kijacho.
Senyi Ngaga namfahamu vizuri, ni dada yetu ambaye wananchi wa
Mbinga tulikuwa na imani naye katika kujenga mshikamano wa kuweza kusukuma
mbele gurudumu la maendeleo, lakini kwa haya yanayoendelea sasa anakatisha tamaa
wananchi anaowaongoza.