Monday, December 3, 2012

POLISI RUVUMA KUFUKUA KABURI ALILOZIKWA KICHANGA


Na Steven Augustino,
Songea.

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma limeahidi kuomba Kibali cha Mahakama ili waweze kufukua kaburi linalodaiwa kuzikwa kitoto kichanga kwa kile kinachoelezwa, kunyimwa na kuzikwa na mama yake Jenister Mapunda (24).

Kuwepo kwa mkanganyiko wa hapa na pale unaoendelea kuzua maneno na taarifa tofauti na kuwachanganya wananchi, ndiko kunakolifanya jeshi hilo kufikia hatua hiyo.

Kamanda wa Polisi wa mkoa huo Deusdedith Nsemeki alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika mahojiano maalumu, na kuongeza kuwa uchunguzi huo pekee ndio utakao ondoa utata na maneno yalityopo sasa.

Nsemeki alieleza kuwa mbali ya maneno ya uzushi kutoka kwa baadhi ya wananchi, pia hali hiyo imetokana na kuwepo kwa taarifa za utatanishi kuwa kabla ya tukio hilo mama huyo alidaiwa kupewa na kumeza dawa, baada ya kushauriwa na Daktari , baada ya kwenda kuomba ushauri kutokana na kusumbuliwa na tumbo.

Alisema pamoja na uchunguzi wa kufukua kaburi hilo pia polisi wanahitaji kujiridhisha  kwa taarifa sahihi kwa daktari aliyempa dawa hizo ambaye hakumtaja jina lake, na kuongeza kuwa pamoja na mambo mengine ni kujiridhisha na taarifa za tukio hilo ikiwa ni pamoja na kupata vielelezo kama mama huyo alikuwa anaenda klinic au la.

Alisema baada ya kukamilisha uchunguzi huo, jeshi hilo litatoa taarifa sahihi kwa wananchi na kuondoa utata huo uliopo sasa, na kuongeza  kuwa usahihi wake pia utatolewa na mwanamume aliyempatia ujauzito huo ambaye atatafutwa na kuhojiwa ili aeleze ni lini mkewe huyo alimwambia kuwa na ujauzito huo.

Kamanda Nsemeki aliendelea kueleza kuwa umuhimu wa taarifa hiyo kutoka kwa mumewe unatokana na uwepo wa taarifa juwa Bi. Mapunda alitokwa na mimba hiyo ya miezi mine, kwa bahati mbaya, huku wengine wakidai alitoa kwa kunywa dawa hizo huku kukiwa na kundi linalodai kuwa mimba hiyo ilifikia wakati wa kujifungua na alijifungua na kukinyonga kitoto hicho.
  
Kwamujibu huyo wa polisi wa mkoa wa Ruvuma, alisema kwa sasa  mama huyo  amelazwa akiwa chini ya ulinzi mkali wa Polisi katika hospitali ya mkoa wa huo, kwa ajili ya matibabu yaliyosababishwa na kutokwa na damu nyingi  wakati
wakujifungua. 

 Sheria itafuata mkondo wake endapo itabainika kuwa alifanya tukio hilo kwa makusudi.

No comments: