Saturday, June 11, 2016

HALMASHAURI YA WILAYA YA MBINGA YAENDELEA KUTEKELEZA ZOEZI LA UFUNGAJI MASHINE ZA EFD'S



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KATIKA kuhakikisha kwamba, Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma inadhibiti vyanzo vyake vya mapato kupitia vituo vya kukusanyia ushuru wa mazao, hivi sasa imenunua mashine za Kieletroniki (EFD’S) ambazo zitatumika kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.

Ujenzi wa jumla ya vituo 13 vya kukusanyia ushuru huo vilivyopo wilayani humo, vitafungwa mashine hizo ambapo jumla ya shilingi milioni 400,000,000 kutoka mapato ya ndani ya halmashauri hiyo, zitatumika katika kukamilisha kazi ya ujenzi wa vituo hivyo na kufungwa mashine za EFD’S.

Hayo yalisemwa juzi na Mweka hazina wa wilaya ya Mbinga, Joseph Mazito wakati alipokuwa akisoma taarifa ya uzinduzi wa kituo cha kukusanyia ushuru wa mazao kilichopo kijiji cha Kihulila wilayani humo, kwa kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, George Mbijima.


Mazito alifafanua kuwa lengo la kufanya hivyo ni kutimiza agizo la serikali la ukusanyaji mapato kwa mfumo wa kieletroniki, kuanzia mwezi Julai mwaka huu na kutoa elimu kwa wananchi wa wilaya hiyo waweze kulipa ushuru na kodi mbalimbali kwa wakati.

Alisema kuwa kufungwa kwa mashine hizo, kutarahisisha huduma za malipo ya mapato kufanyika kwa wakati na kuweza kuokoa muda wa kufanya shughuli nyingine za maendeleo ya wananchi.

Alieleza kuwa, mfumo huo wa EFD’S utaweza kuongeza ukusanyaji wa mapato ya ndani ya halmashauri na kudhibiti mianya ya upotevu wa mapato hayo.

Hata hivyo kwa upande wake kiongozi wa mbio za Mwenge wa uhuru kitaifa Mbijima, alipongeza jitihada hizo zinazofanywa na halmashauri hiyo kwa kudhibiti mapato hayo huku akiutaka uongozi husika kuhakikisha kwamba, kazi hiyo inafanywa kikamilifu na kuwa endelevu kwa manufaa ya jamii kwa kuelekeza fedha hizo zinazopatikana kupitia makusanyo hayo kwenda kutekeleza miradi ya maendeleo ya wananchi.

No comments: