Thursday, June 16, 2016

WANANCHI WASHAURIWA KUWA NA MAZOEA YA KUTUNZA MIRADI INAYOTEKELEZWA NA SERIKALI

Kiongozi wa mbio za Mwenge uhuru mwaka 2016, George Mbijima upande wa kulia akikabidhi chandarua chenye dawa kwa  mkazi wa kijiji cha Mbuji kata ya Mbuji wilayani Mbinga Sailice Komba ikiwa ni mpango wa halmashauri ya wilaya hiyo kutokomeza ugonjwa wa Malaria kwa wananchi wake, kati kati ni Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Venance Mwamengo. Tukio hilo la kukabidhi chandarua lilifanyika juzi wakati Mwenge huo ulipowasili wilayani hapa, kwa ajili ya kutembelea miradi ya aina mbalimbali ya kimaendeleo.


Na Muhidin Amri,
Mbinga.

WANANCHI mkoani Ruvuma, wamehimizwa kuwa na tabia ya kutunza miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na serikali kwa fedha nyingi, yenye lengo la kuharakisha kukua kwa uchumi wa  mkoa huo na taifa kwa jumla.

Aidha wametakiwa kuacha kuhujumu miradi hiyo, ili kuepusha uwezekanao wa kukatisha tamaa baadhi ya wahisani ambao  wanajitolea fedha zao nyingi kujenga miundombinu husika, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za serikali katika kukabiliana na changamoto zilizopo hasa katika utoaji wa huduma muhimu za kijamii.

Wito huo umetolewa juzi na kiongozi wa mbio za Mwenge wa uhuru kitaifa George Mbijima, alipokuwa akifungua zahanati ya kijiji cha Kihulila wilayani Mbinga ambayo ilijengwa  kwa  fedha za mapato ya ndani ya halmashauri ya wilaya hiyo, ili kuwaondolea kero wakazi wa kijiji hicho na maeneo ya jirani kutembea umbali mrefu kufuata huduma za afya.


Mbijima alisema kuwa siku zote serikali ndiyo inayotoa fedha  za kukamilisha ujenzi wa mradi wowote ule, huku akisema kuwa hata zahanati hiyo ambayo ilianza kujengwa mwaka  2008 kuna kila sababu kwa wananchi kuitunza ili iwe endelevu na kusaidia katika suala zima la  kuharakisha maendeleo katika maeneo yao.

Alisema kuwa licha ya serikali kutumia fedha nyingi kutekeleza miradi mbalimbali  ya kimaendeleo lakini bado kuna fikra  potofu, iliyojengeka miongoni mwa  watu wachache hapa nchini kwamba kila jambo linalofanywa na serikali wananchi hawapaswi kuitunza au kuunga mkono kitendo ambacho kiongozi huyo wa mbio za mwenge alikemea na kuitaka jamii kuachana na hali hiyo.

Kwa mujibu wa Mbijima alieleza kwamba, kuhujumu miradi hiyo ni sawa na kujiua wenyewe kwa sababu inatekelezwa kwa kutumia kodi za wananchi kwa manufaa ya kizazi cha sasa na baadae.

No comments: