Saturday, June 4, 2016

WANANCHI WAILALAMIKIA TANROADS KWA KUTOFANYIA MATENGENEZO BARABARA KWA MUDA MREFU



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WANANCHI waishio katika kata ya Kitura wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wameulalamikia uongozi wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mkoani humo kwa kushindwa kufanyia matengenezo kwa muda mrefu barabara ya kutoka kata ya Litembo hadi kijiji cha Nkili wilayani Nyasa, jambo ambalo limekuwa likisababisha kero kubwa kwao hasa pale wanaposafirisha wagonjwa au mazao yao kutoka shambani.
Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu.

Barabara hiyo ambayo ina zaidi ya kilometa 30 walisema, kutokana na kuwa katika hali mbaya wamekuwa wakati mwingine wakilazimika kutumia jembe la mkono kuitengeneza, hasa nyakati za masika magari yao yanapokuwa yanakwama barabarani.

Malalamiko hayo yalitolewa juzi na wananchi hao, kwenye kikao cha baraza la kata kilichofanyika kwenye ofisi ya makao makuu ya kata ya Kitura wilayani Mbinga na kuhudhuriwa na Diwani wa kata hiyo, Alex Ngui ambacho kililenga kujadili maendeleo ya kata hiyo.


Walifafanua kuwa katika kipindi hicho cha masika, hata wanaposafirisha wagonjwa wao hulazimika kuwabeba kwenye machela kuwapeleka hospitali ya Litembo, ambayo ipo jirani na kata hiyo kutokana na magari kushindwa kupita kufuatia barabara hiyo kuwa katika hali mbaya.

Walieleza kuwa wanamuomba Mkuu wa mkoa huo Said Mwambungu, aingilie kati kutatua kero hiyo ili kuweza kunusuru tatizo hilo lisiendelee kutesa wananchi ukizingatia kwamba, kata hiyo pia ina wakulima wengi ambao wamekuwa wakizalisha zao la kahawa kwa wingi ambalo limekuwa likiingizia serikali mapato makubwa.

“Sisi tunaiomba serikali isikilize kilio chetu cha kutengeneza barabara hii ni miaka mingi imepita hakuna utekelezaji uliofanyika, tumekuwa tukijitolea kuchimba kwa jembe la mkono ili watu waweze kupita kwa muda”, walisema.

Kwa upande wake akizungumza katika kikao hicho, Diwani wa kata ya Kitura Ngui aliongeza kuwa hata barabara ambazo inabidi zihudumiwe na halmashauri hiyo kwa ajili ya matengenezo ya kila mwaka, zina hali mbaya na ni kikwazo kikubwa katika usafirishaji wa mazao ya wakulima kutoka shambani kwenda kwenye masoko.

Hata hivyo Ngui alisema kwamba tatizo hilo atalifikisha kwa uongozi husika wa wilaya na mkoa, ili liweze kupatiwa ufumbuzi wa kudumu na wananchi wake waweze kuondokana na kero hiyo ambayo inaendelea kuwatesa kwa muda mrefu na kurudisha nyuma maendeleo ya wananchi wake.

No comments: