Sunday, June 5, 2016

MBINGA WAIOMBA WIZARA YA MAJI NA UMWAGILIAJI KUPANUA MRADI WA MAJI

Mji wa Mbinga ambao hivi sasa unakua kwa kasi.


Na Muhidin Amri,
Mbinga.

WANANCHI wanaoishi katika mji wa Mbinga mkoani Ruvuma wameiomba serikali kupitia Wizara ya maji na Umwagiliaji, kuchukua hatua katika mipango yake kupanua mradi wa maji safi na salama katika mji huo, hatua ambayo itawezesha wananchi wengi kupata huduma ya maji safi na salama.

Ushauri huo ulitolewa na wananchi hao walipokuwa wakizungumza na mwandishi wetu kwa nyakati tofauti, kufuatia hivi sasa wamekuwa wakitumia muda mwingi kwenda umbali mrefu kutafuta huduma ya maji hayo kwa ajili ya matumizi mbalimbali majumbani kwao.

Walisema kuwa hali hiyo inatokana na miundombinu inayotumika sasa kuchakaa na wakati mwingine huharibika mara kwa mara, jambo ambalo limekuwa likiwafanya kupata maji kwa mgao na kuwa kero kubwa kwao.


Walifafanua kuwa serikali kupitia Mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira katika mji wa Mbinga (MBIUWASA) umefika wakati sasa, kuchukua hatua ya kuipatia ruzuku ya fedha itakayoweza kuifanya mamlaka hiyo kuboresha miundombinu yake ya maji katika mji huo, ili wananchi waweze kuondokana na adha wanayoipata sasa.

Dickson Ndunguru ambaye ni mkazi wa Mbinga mjini alisema kwamba hali ya upatikanaji wa maji katika mji huo hasa kwa kipindi cha kiangazi imekuwa ni vigumu upatikanaji wake, licha ya ukweli kwamba mji wa Mbinga umezungukwa na mito na mifereji mingi ambayo hutiririsha maji kipindi cha mwaka mzima.

Kwa upande wake Meneja MBIUWASA Patrick Ndunguru, alipohojiwa juu ya hali hiyo alisema kuwa kero hiyo ya uzalishaji mdogo wa maji inatokana na kuchakaa kwa miundombinu ya kuleta na kusambaza maji katika mji huo, kutoka kwenye chanzo kikuu cha Ndengu kilichopo kijiji cha kihereketi kata ya Nyoni wilaya ya Mbinga.

“Ni kweli tuna upungufu mkubwa wa maji katika mji wetu, tatizo hili linachangiwa kwa kiasi kikubwa na ukosefu wa fedha hivyo kama serikali itasaidia Mamlaka kuipatia fedha za kutosha tutaweza kuboresha miundombinu husika iweze kuwa ya kisasa zaidi, ambayo itazalisha maji mengi yanayotosheleza mahitaji ya wakazi wa mji wa Mbinga”, alisema Ndunguru.

No comments: