Sunday, April 1, 2018

BREAKING NEWS: MZIMU WA UBADHIRIFU FEDHA ZA WANACHAMA WAENDELEA KUITAFUNA MBINGA TEACHERS SACCOS

Baadhi ya Wanachama wa Mbinga Teachers SACCOS, Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma wakiwa jana kwenye Mkutano wao wa uchaguzi, ambao haukufanyika kutokana na idadi kamili ya wanachama wenzao kutotimia.

Na Kassian Nyandindi,        
Mbinga.

MKUTANO Mkuu wa uchaguzi wa kuwachagua Viongozi wapya wa Chama cha Akiba na Mikopo, Mbinga Teachers SACCOS Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma jana Machi 31 mwaka huu, umeshindwa kufanyika kutokana na idadi kamili ya Wanachama wa Chama hicho kushindwa kuhudhuria katika mkutano huo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti ndani ya ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa ambako Mkutano huo ulitarajiwa kufanyika hapo, baadhi ya Wanachama wa chama hicho walisema kuwa tatizo hilo limesababishwa na wanachama wenzao kukata tamaa ya kuendelea kuwa wanachama ndani ya ushirika huo kutokana na ubadhirifu wa mamilioni ya fedha, uliofanywa na viongozi husika waliopewa dhamana ya kuendesha umoja wao.

Walisema kuwa licha ya kutoa kilio chao kwa muda mrefu wakitaka vyombo vya dola na Serikali kwa ujumla, iingilie kati kupitia Mrajisi wa Vyama vya ushirika Mkoani Ruvuma ili kuweza kunusuru mali na fedha zao, hali hiyo bado imekuwa mbaya na ndiyo maana wamekata tamaa.


Adolph Komba ambaye ni mwanachama wa chama hicho na pia Mwalimu wa shule ya msingi Luwino iliyopo kata ya Mkumbi Wilayani hapa, alifafanua kuwa Maafisa ushirika wamekuwa ndiyo chanzo cha ubadhirifu wa fedha zao ambapo wamekuwa wakiendekeza vitendo vya rushwa na kusimamia utoaji wa mikopo isiyofuata taratibu na miongozo ya ushirika.

“Hata mimi binafsi nimekuwa nikishangazwa na jambo moja, nimekuwa nikikatwa fedha katika mshahara wangu wakati sina mkopo na sikukopa popote, lakini kila nikifuatilia namna ya kusitisha mkopo ule na kurejeshewa fedha zangu zilizokatwa kimakosa hakuna shirikiano na utekelezaji ninaoupata, nimekuwa nikizungushwa kila siku kwa kweli hali ya chama chetu ni mbaya kuliko kama mnavyofikiria”, alisema Komba.

Komba aliongeza kuwa kutokana na hali hiyo husababisha maendeleo ya chama hicho na yawanachama kwa ujumla wao kurudi nyuma, hivyo kuna kila sababu sasa viongozi wa ngazi ya juu Serikalini kuingilia kati kupitia Mrajisi wao wa Mkoa huo, kuingilia kati na kuchukua hatua kali za kisheria juu ya kumaliza matatizo hayo yaliyopo.

Vilevile imeelezwa kuwa watumishi ambao waliajiriwa katika chama hicho, wanalalamikiwa wakidaiwa kutofuata taratibu husika za utoaji wa mikopo na kutoandaa taarifa za hesabu kikamilifu kwa muda unaotakiwa.

Naye Charles Makenziye ambaye ni mwanachama wa ushirika huo alieleza kuwa pia kumekuwa na madeni makubwa ndani ya chama chao, kufuatia taasisi ya kifedha benki ya CRDB kuikopesha SACCOS hiyo na kwamba mzigo wa madeni hayo umesababishwa na utendaji mbovu wa watendaji waliokuwa madarakani katika chama hicho kwa kutozingatia taratibu husika.

Pia aliinyoshea kidole iliyokuwa bodi ya mikopo ikilalamikiwa kwamba imekuwa haikuzingatia ushauri unaotolewa na idara ya ushirika Wilayani Mbinga na ndiyo maana chama hicho kinaenda mrama.

Vilevile mikopo ambayo chama ilikopa toka taasisi hiyo ya fedha imefikia hatua kutoingia kwenye mzunguko husika na hali hiyo imesababisha sasa kutumia mtaji wa ndani kulipia madeni ya nje na kukifanya kishindwe kusonga mbele kimaendeleo.

Naye Mjumbe wa bodi ya Mbinga Teachers SACCOS, Aderick Kapinga aliwasihi wanachama wenzake akiwataka kuwa watulivu na kupanga siku nyingine ya kuweza kufanya Mkutano huo na kuweza kufikia suluhisho la matatizo hayo, ikiwemo kuwachagua viongozi wengine wapya watakaoweza kuongoza chama hicho.

Pamoja na mambo mengine naye Afisa ushirika anayesimamia vyama hivyo vya akiba na mikopo hapa Mbinga, Erasto Msanga alisisitiza kwa kuwataka wapange tarehe nyingine ambapo walifikia maamuzi kwamba Mkutano huo waufanye Aprili 28 mwaka huu na kwamba, matangazo yawafakie wanachama wote kwa wakati ili waweze kuhudhuria siku hiyo kwa wingi na kuweza kufanikiwa taratibu husika za kuweza kuwachagua viongozi hao wapya.


No comments: