Tuesday, April 24, 2018

WANACHAMA WA USHIRIKA TUNDURU WAASWA


Na Dustan Ndunguru,    
Tunduru.

VIONGOZI wa vyama vya ushirika Wilayani Tunduru, Mkoa wa Ruvuma wametakiwa kusimamia kikamilifu hesabu za vyama hivyo, ili viweze kuwanufaisha wanachama wake na kuvifanya kuwa endelevu.

Mkuu wa Wilaya hiyo, Juma Homera alisema kuwa viongozi wengi wa vyama ushirika hapa nchini wamekuwa legelege katika kufuatilia mikopo wanayotoa kwa wanachama wao, na kushindwa kusimamia hesabu ipasavyo za uendeshaji wa ushirika huo na mwisho wa siku husababisha kuyumba na kufa kabisa kwa vyama vya ushirika.

Alisema kuwa wanachama wa vyama hivyo wanatakiwa kujenga mazoea ya kulipa mikopo waliyokopeshwa kwa wakati, ili kuweza kutoa nafasi kwa wanachama wengine waweze kukopa.


Homera alisisitiza kuwa imekuwa ni mazoea miongoni mwa wanachama kuona fahari kwamba fedha wanazokopa kuwa ni mali yao, kwa kutoirejesha kwenye vyama hivyo jambo ambalo linarudisha nyuma maendeleo husika.

Alisema kuwa ni aibu kwa mwanachama kufukuzwa ndani ya ushirika baada ya kushindwa kurejesha mkopo aliokopa kwa hiari yake bila kulazimishwa, jambo ambalo halipendezi kwa sababu linaondoa imani na uaminifu wake hususan katika vyombo fedha kama vile benki.

Mkuu huyo wa Wilaya Tunduru aliwataka pia wanachama hao kutumia vyema mikopo wanayokopeshwa na kwamba waepuke vitendo vya anasa ambavyo huwafanya washindwe kuondokana na umaskini unaowakabili miongoni mwao.

Alisema dhamira kubwa ya Serikali ya awamu ya tano ni kuona vyama vyote vya ushirika vinafanya kazi kwa umakini mkubwa ili wananchi waweze kunufaika navyo huku akongeza kuwa haitasita kuwachukulia hatua za kisheria wale wote watakaonekana kutaka kuzorotesha maendeleo ya ushirika.

No comments: