Tuesday, April 24, 2018

RC RUVUMA AWATAKA VIONGOZI WAZAZI KUPIGA VITA MIMBA ZA UTOTONI


Na Kassian Nyandindi,   
Songea.

SERIKALI katika kipindi cha kuanzia mwezi Julai mwaka jana hadi kufikia Machi mwaka huu, tayari imetumia jumla ya Shilingi bilioni 4,894,932.063 Mkoani Ruvuma kwa ajili ya kuboresha mazingira ya elimu.
Christine Mndeme.

Aidha huo ni mkakati wake wa kuwezesha mpango wa elimu bila malipo kwa shule za Msingi na Sekondari Mkoani humo uweze kuwa endelevu.

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme alisema hayo alipokuwa akizungumza na Wadau mbalimbali wa elimu Mkoani hapa katika kikao cha tathimini ya elimu kilichoketi kwenye ukumbi wa Manispaa ya Songea mjini hapa.

Alisema kuwa ni jambo la kumshukuru Rais Dkt. John Magufuli kwa jitihada zake za kuboresha mazingira ya elimu hapa nchini ambapo ameweza pia kutoa vifaa vya maabara kwenye shule za Serikali, jambo ambalo sasa linasaidia watoto shuleni waweze kusoma masomo ya Sayansi kwa vitendo bila usumbufu wa aina yoyote ile.


Hatua hiyo Mndeme alieleza kuwa imewezesha wanafunzi hao kufanya vyema katika masomo na mitihani yao hatimaye kuweza kuondokana na aibu ya watoto kuendelea kufanya vibaya.

Katika matokeo ya mitihani ya miaka mitatu iliyopita ufaulu katika Mkoa huo umekuwa ukishuka, kwani matokeo ya darasa la saba kutoka yalikuwa asilimia 68.4 mwaka 2015 hadi asilimia 66.26 mwaka 2016 na asilimia 64.2 mwaka 2017.

Alisema kutokana na ufaulu huo Mkoa umeshuka kutoka nafasi ya 11 mwaka 2015 na kushika nafasi ya 16 mwaka 2016, hadi kufikia nafasi ya 21 katika ngazi ya kitaifa mwaka 2017, huku asilimia ya ufaulu kwa mitihani ya darasa la saba mwaka 2016 ilikuwa asilimia 66.28 hivyo kupungua kwa asilimia 2.08 mwaka 2017.

Kwa upande wa mitihani ya kidato cha nne Mndeme alisema ufaulu umekuwa sio imara toka asilimia 74.58 ya mwaka 2015, asilimia 82.29 mwaka 2016 hadi asilimia 77.28 ya mwaka 2017 huku mwaka 2015 Mkoa ukishika nafasi ya 7, nafasi ya nane mwaka 2016 na nafasi ya 25 kati ya mikoa 30 mwaka 2017.

Mndeme aliongeza kuwa changamoto kubwa iliyosababisha kuwa na matokeo mabaya ni utoro, ufundishaji usiokidhi viwango, viongozi katika ngazi mbalimbali kutofanya ufuatiliaji, upungufu wa baadhi ya vifaa vya kujifunzia, kufundishia na mimba za utotoni kwa watoto wa kike.

Katika kukabiliana na tatizo la mimba Mkuu huyo wa mkoa amepiga marufuku walimu na wakuu wa shule zote za Msingi na Sekondari kuwapokea wanafunzi waliopata ujauzito, ambapo ameitaka jamii kuhakikisha kwamba wanapambana kupiga vita mimba za utotoni ili kutoa fursa kwa wanafunzi wa kike waweze kusoma na hatimaye kutimiza ndoto zao.

No comments: