Sunday, April 1, 2018

UHAMASISHAJI ELIMU YA KUJITOLEA DAMU NI LAZIMA



Na Albano Midelo,    
Songea.

MANISPAA ya Songea Mkoani Ruvuma kwa kushirikiana na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa huo, wiki ya mwisho wa mwezi Machi mwaka huu iliweka kituo cha wananchi kujitolea damu katika viwanja vya Soko kuu mjini Songea. 

Uchunguzi umebaini kuwa asilimia 80 ya wanaohitaji damu hapa nchini ni wanawake, kwa sababu mbalimbali ikiwemo uzazi salama wakati wa kujifungua kwa njia ya kawaida na njia ya upasuaji. 

Katika kipindi cha siku tatu za uhamasishaji wa wananchi kujitolea damu, lengo lilikuwa ni kukusanya uniti 100 za damu.


Vilevile kuanzia Machi 27 hadi 29 mwaka huu kitengo cha damu salama katika kituo cha Soko hilo kilikuwa kimekusanya uniti 67.

Changamoto kubwa iliyosababisha kutofikia malengo ya kukusanya uniti 100 kwa siku tatu ni kutokana na kufungwa kwa shule za Sekondari, kwa ajili ya kwenda mapumziko ya sikukuu ya Pasaka hali ambayo imesababisha watu wachache kujitolea damu salama.

Kadhalika imebainika kuwa watu wanaoongoza kujitolea kutoa damu ni wanafunzi wa shule za Sekondari na taasisi zingine kama vile Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).

Jambo la msingi ni kuendelea kutoa elimu ya kujitolea damu kwa Watanzania kwa kutumia vyombo vya habari, matangazo, mikutano ya hadhara hali ambayo itaweza kuhamasisha wananchi wengi kwa kiasi kikubwa kuona umuhimu wa kujitolea damu ili vituo vya afya na hospitali ziweze kuwa na benki ya kutosha ya damu salama.

Mpango wa Taifa wa damu salama umesema kuwa Jamii Kutokuwa na elimu ya kutosha juu ya umuhimu wa kujitolea damu, imekuwa ni kikwazo kikubwa namba moja kwa mpango huo kushindwa kufikia malengo ya ukusanyaji wa damu salama kutoka kwa wananchi.

Kuna wale wanaoamini kwamba kujitolea damu ndiyo mwanzo wa kubomoa mfumo sahihi wa mzunguko wa damu na kuna wanaoamini kuwa kujitolea damu ndiyo kujiletea ugonjwa wa shinikizo la damu.

Fikra hizo ndizo zinanidhihirishia wazi kuwa katika umma huu wa Watanzania, wapo wasioelewa mambo mengi muhimu kuhusu kujitolea damu, hivyo kusababisha utoaji damu kwa hiyari kuwa mgumu.

Kuna umuhimu sasa wahusika waliopewa dhama kutekeleza jambo hilo kuweka utaratibu mzuri, wa kuhakikisha elimu sahihi kuhusu umuhimu wa watu kujitolea damu inawafikia hata wananchi wanaoishi vijijini.

Maneno hayo yanayozungumzwa na wasioelewa kuhusu umuhimu wa kutoa damu ni mengi, kwa hiyo wahusika waichukulie hiyo kuwa ni changamoto kubwa inayopaswa kutafutiwa ufumbuzi wa kudumu ili hatimaye, tatizo la upungufu wa damu katika vituo vyetu vya kutolea huduma za afya libakie kuwa historia.

No comments: