Saturday, April 21, 2018

MANISPAA SONGEA WAPATIWA MAFUNZO UTOAJI CHANJO SARATANI MLANGO WA KIZAZI

Walimu wa afya katika shule za Msingi na Sekondari na Wahudumu wa afya kutoka katika Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, wakipata mafunzo ya utoaji wa chanjo ya Saratani mlango wa kizazi katika ukumbi wa Manispaa hiyo, ili waweze kwenda kuwahudumia Watoto wenye umri kuanzia miaka tisa hadi 14.

Na Kassian Nyandindi,     
Songea.

MAFUNZO ya utoaji wa Chanjo ya Saratani mlango wa kizazi, kwa wasichana wenye umri kuanzia miaka tisa hadi 14 yamefanyika katika Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma.

Aidha mafunzo hayo yameshirikisha Walimu wa afya kutoka shule za Msingi na Sekondari na Wahudumu wa afya ya msingi zaidi ya 300 kutoka katika Manispaa hiyo mjini hapa.

Kufanyika kwa zoezi hilo kunalenga kwamba kabla ya siku ya Jumatatu Aprili 23 mwaka huu, siku hiyo utafanyika uzinduzi wa Mkoa huo wa chanjo hiyo kwa wasichana wenye umri huo.


Uzinduzi huo kimkoa unatarajiwa kufanywa na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme.

Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa huo, Dokta Mameritha Basike alisema hayo leo wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Songea, Tina Sekambo.

Dokta Basike amelitaja lengo la Manispaa hiyo ni kutoa chanjo ya Saratani mlango wa kizazi kwa wasichana 1,834 na kwamba lengo la Mkoa ni kutoa chanjo hiyo kwa wasichana 28,676.

“Manispaa ya Songea tumejipanga kuhakikisha kuwa tunatoa chanjo hii kwa asilimia kati ya 99 hadi 100, zoezi hili katika Mkoa wetu litaanza Aprili 23 hadi 29 baada ya hapo zoezi hili la utoaji chanjo ya Saratani mlango wa kizazi litakuwa endelevu”, alisema Dokta Basike.

Alisema kuwa chanjo hiyo ni muhimu kwa sababu itapambana na Virusi vinavyoitwa Human Papiloma Virus (HPV) ambavyo huambukizwa kwa njia ya ngono na kwamba chanjo inakusudia kuweka kinga dhidi ya kirusi hicho ambacho kinasababishwa na kufanya ngono hasa katika umri mdogo.

Mmoja wa watoa mada katika mafunzo hayo, Flowin Komba amevitaja visababishi vya Saratani hiyo ni kuanza ngono katika umri mdogo, kufanya ngono na wapenzi wengi, historia ya kubeba mimba nyingi na uvutaji wa sigara, tumbaku na ugoro.

Takwimu zinaonesha kuwa kila mwaka wagonjwa 6,000 wa Saratani mlango wa kizazi na matiti wanagundulika kuwa na magonjwa hayo huku kati yao wagonjwa 4,000 hupoteza maisha.

Takwimu kutoka Taasisi ya Saratani ya Ocean Road iliyopo Jijini Dar es Salaam, inaonesha kwamba mwaka 2015 Tanzania ilikuwa na wagonjwa wa Saratani 2,500 ambapo mwaka huo idadi hiyo, iliongezeka hadi kufikia 5,200 sawa na ongezeko la asilimia 100.

Kulingana na takwimu hizo Saratani ya mlango wa kizazi na matiti husababisha asilimia 50 ya vifo, vinavyotokana na Saratani kwa akina mama na kwamba kila watu 100 wanaochunguzwa hubainika wagonjwa 36 kuwa na Saratani.

No comments: