Thursday, November 10, 2016

ASKOFU NDIMBO: WANAUME WANAOKATISHA MASOMO WANAFUNZI WA KIKE WAPEWE ADHABU KALI

Na Mwandishi wetu,          
Mbinga.

ASKOFU wa Kanisa katoliki jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma, John Ndimbo ameitaka serikali ya awamu ya tano kutokuwa na huruma kwa wanaume ambao wanakatisha masomo ya wanafunzi wa kike waliopo mashuleni kwa kuwapa mimba huku wengine wakidiriki kuwaoa, kwani ni wakati sasa wa kuwachukulia hatua na adhabu kali za kisheria ili iweze kuwa fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Askofu John Ndimbo.
Vilevile alisema kuwa vitendo hivyo licha ya kuwa havimpendezi Mungu, vimekuwa vikikatisha ndoto za watoto wengi wa kike hapa nchini na kurudisha nyuma maendeleo yao sasa umefika wakati wa kutofumbia macho hali hiyo.

Askofu Ndimbo alitoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki wakati alipokuwa akizungumza na madiwani, watumishi na baadhi ya wananchi waliohudhuria kikao cha baraza la madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga kilichoketi kwenye ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa.


Alieleza kuwa baadhi ya wanaume tena wenye umri mkubwa, wakiwemo walimu na watumishi wengine wa serikali wamekuwa na tabia mbaya ya kufanya mapenzi na watoto hao ambao bado wanaendelea na masomo shuleni jambo ambalo limekuwa likikatisha ndoto zao na matumaini ya wasichana wengi, katika maendeleo yao ya sasa na baadaye.

Pamoja na mambo mengine Askofu huyo ameishauri serikali kupitia halmashauri za wilaya, kuiangalia kwa jicho la huruma shule ya msingi Kitulo iliyopo wilayani hapa ambayo ina hali mbaya ambapo kuta zake zimejenga nyufa, kupasuka kwa milango, madirisha na walimu kukosa hata sehemu ya ofisi yenye hadhi ambayo inaweza kuwafanya wafanye kazi kwa moyo wa kujituma.

Sambamba na hilo Askofu Ndimbo alibainisha kuwa ni muhimu sasa kwa serikali kufanya upendeleo wa kutenga kiasi cha fedha ili kuifanyia ukarabati shule hiyo ambapo hata walimu wake, wameonekana kukata tamaa kutokana na hali mbaya ilivyo jambo ambalo linawafanya washindwe kutekeleza wajibu wao kikamilifu na kurudisha nyuma kiwango cha taaluma.

Kadhalika amewataka Madiwani wa wilaya ya Mbinga kuendeleza umoja wao kwa kujenga ushirikiano na kuvumiliana kwa kufanya kazi pamoja kama mchwa na kuweka kando tofauti zao za vyama vya kisiasa.

Mbali na pongezi hizo pia Askofu Ndimbo alisisitiza kuwa ni wakati sasa wa kuwa makini katika usimamizi na ufuatiliaji wa fedha zinazotengwa kwa ajili ya kuboresha huduma za jamii katika kata zao, ikiwemo kuwashirikisha wananchi wao na kuwahimiza kujenga ushirikiano katika kuibua na kutekeleza miradi ya maendeleo katika maeneo yao.

No comments: