Saturday, November 5, 2016

TUNDURU WAANZISHA OPARESHENI MAALUM YA KUKABILIANA NA UPUNGUFU WA MAJENGO

Na Muhidin Amri,       
Tunduru.

WILAYA ya Tunduru  mkoani Ruvuma, imeanza Operesheni maalum ya kukabiliana na upungufu wa majengo ya umma ambapo hivi sasa ufyatuaji wa tofari 100,000 kwa kila kijiji unafanyika,  ili kuweza kupata matofari ya kujengea majengo ya shule kama vile madarasa, nyumba za walimu, zahanati na vyoo.

Akiwa katika hafla ya kukabidhi matofari 7,642,816 kwa Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge katika vijiji vya Ligoma na Makoteni, Mkuu wa wilaya ya Tunduru Juma Homera alisema kuwa, baada ya kubaini  wilaya yake ina upungufu mkubwa wa majengo hayo ya umma wameamua kuanzisha operesheni hiyo ili kuweza kufikia malengo husika.

Homera alimweleza Dkt. Mahenge kuwa matofari hayo ni ya awali tu na kwamba katika baadhi ya vijiji wananchi wanaendelea na kazi hiyo, ambapo vijiji vingine wilayani hapa vipo katika hatua ya kuchoma tofari hizo na kwamba zoezi hilo litakapokamilika wanatarajia kuwa na tofari 16,700,000.


Alibainisha kuwa hadi sasa tarafa ya Mlingoti imekabidhi matofali 1,901,842 tarafa ya Matemanga 690,000 Namasakata 1,204600 Nalasi 1,365974 Lukumbule 955,000 Nakapanya 830,000 na Nampungu tofari 695,400.


Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Mahenge alipongeza jitihada hizo zinazofanywa na wananchi wa wilaya ya Tunduru na kuongeza kuwa waendelee kujitokeza kuchangia nguvu zao katika shughuli za maendeleo, ili kuweza kukuza uchumi wa wilaya na taifa kwa ujumla.

No comments: