Saturday, November 12, 2016

CHADEMA WAFUKUZANA UANACHAMA SONGEA FUIME ADAIWA KUKALIA KUTI KAVU

Joseph Fuime akiwa katika majukwaa ya mikutano ya siasa mjini Songea iliyofanyika hivi karibuni.
Na Gideon Mwakanosya,           
Songea.

CHAMA Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, kimemvua uanachama Joseph Fuime akidaiwa kufanya makosa mbalimbali ikiwemo kukihujumu chama hicho wakati alipokuwa mgombea ubunge kupitia tiketi ya CHADEMA jimbo la Songea mjini, katika uchaguzi mkuu uliopita Oktoba 25 mwaka jana.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Ofisini kwake, Katibu wa CHADEMA wilaya ya Songea, Olais Ng`ohison alisema kuwa Fuime amefutwa kwenye orodha ya kuwa mwanachama wa chama hicho, tangu Octoba 23 mwaka huu na kwamba  hivi sasa sio mwanachama tena wa chama hicho.

Alisema kuwa chama hicho kimelazimika kutoa taarifa kupitia vyombo vya habari kuwajuza wananchi, wadau, wakereketwa pamoja na viongozi mbalimbali wa serikali baada ya kubaini kwamba watu wengi walikuwa hawafahamu kuondolewa na kufutwa uanachama kwa Fuime.


Kadhalika alifafanua kuwa Fuime katika kipindi cha uchaguzi mkuu wa mwaka jana alikuwa mgombea ubunge kwa tiketi ya chama hicho, lakini alikihujumu chama kwa mambo mbalimbali yakiwemo ya kutoshiriki katika majumuisho ya kura kwenye ukumbi wa halmashauri ya Manispaa ya Songea na kuamua kuzima simu zake zote za kiganjani bila sababu za msingi.

Ng`ohison alifafanua zaidi kuwa hujuma nyingine alizozifanya ni kutokabidhi nakala halisi za matokeo ya uchaguzi huo, tangu uchaguzi mkuu wa mwaka jana umalizike kufanyika na badala yake alileta nakala (vivuli) 318 kati ya 324 baada ya miezi 8 kupita na kukidanganya chama kwamba, kura alizokuwa amepata kwenye uchaguzi huo ni 37,012 wakati kwa mujibu wa nakala au vivuli 318 zinaonesha kuwa alipata kura 40,786 jambo ambalo lilikuwa likileta utata mkubwa ndani ya chama na wanachama kwa ujumla.

Kutokana na hali hiyo alisema amesababisha kuathiri ruzuku ya chama katika ngazi zote kutokana na udanganyifu wa kura alioufanya na kwamba alipoandikiwa na chama hakuweza kujibu na alikataa kufika kwenye kikao cha kamati tendaji ambacho kilitaka kumhoji juu ya tuhuma hizo na aweze kuzitolea ufafanuzi wa kina.

Alisema kwamba kufuatia hujuma hizo kamati tendaji ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo wilaya ya Songea imeamua kumfukuza uanachama Fuime huku chama kikiwataka wadau wake wote kutoshirikiana naye katika maswala yoyote yanayohusu chama hicho ndani na nje ya wilaya ya songea.


Kwa upande wa waandishi wa habari walipofanya mawasiliano na Joseph Fuime na kumtaka atoe ufafanuzi juu ya kufukuzwa kwake kwenye chama hicho alisema kuwa hatambui juu ya kufukuzwa huko, bali anachofahamu yeye ni bado mwanachama wa CHADEMA huku akiongeza kuwa kadi yake ya uanachama ameilipia hadi mwaka 2020 ambayo bado anaendelea kuimiliki.

No comments: