Monday, November 28, 2016

SERIKALI YAOMBWA KUINUSURU HOSPITALI YA MISHENI MBESA TUNDURU

Na Kassian Nyandindi,        
Tunduru.

HOSPITALI kongwe ya Misheni Mbesa ambayo inamilikiwa na Kanisa la Bibilia Tanzania wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, ipo katika hali mbaya yenye kuhatarisha kufungwa wakati wowote kuanzia sasa kutokana na Madaktari kutoka nje ya nchi ambao walikuwa ni tegemeo kubwa katika kuendesha hospitali hiyo kuanza kufunga virago kurejea makwao, baada ya mikataba yao ya kufanya kazi kwisha.

Hospitali ya Misheni Mbesa.
Katibu tawala wa hospitali hiyo, Dkt. John Mwaya alisema hayo wakati alipokuwa akitoa taarifa ya maendeleo ya hospitali yake kwa Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Juma Homera ambaye alifanya ziara ya kutembelea hospitali hiyo kwa lengo la kujionea maendeleo mbalimbali.

Dkt. Mwaya alibainisha kuwa changamoto kubwa inayotishia kufa kwa hospitali yake ni kuwepo kwa upungufu wa Madaktari wenye taaluma na wauguzi walio somea fani hiyo ili kuweza kutosheleza ikama husika.


Alisema kuwa hospitali ya Mbesa ambayo ni tegemeo kubwa kwa wananchi waishio wilayani Tunduru na nje ya wilaya hiyo tangu mwaka 1957 kuna kila sababu kwa serikali, kuchukua jitihada za makusudi katika kuinusuru kwa kupeleka wataalamu wa fani za kitabibu pamoja na kuipunguzia mzigo wa kuwalipa mishahara baadhi ya watumishi wenye sifa watakaohudumia hospitalini hapo.

Naye Kaimu Mkuu wa shirika la Misheni Mbesa, Heiga Armbruster alipongeza ujio wa Mkuu wa wilaya hiyo na kueleza kuwa anayoimani kwamba kero hizo zitatatuliwa na kuifanya hospitali iweze kuendelea kutoa huduma kwa wagonjwa wanaohitaji matibabu.

Akijibu kero hizo Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Juma Homera aliwataka viongozi wa hospitali hiyo kuorodhesha changamoto zinazowakabili na kuzipeleka haraka Ofisini kwake, ili aweze kuwasiliana na Waziri mwenye dhamana kwa lengo la kuyatafutia ufumbuzi.

No comments: