Thursday, November 10, 2016

POLISI TUNDURU KUWAKAMATA WAPIKA GONGO NA KUWAFIKISHA MAHAKAMANI

Na Mwandishi wetu,                   
Tunduru.

MKUU wa wilaya ya Tunduru Juma Homera, ameliagiza Jeshi la Polisi wilayani hapa kuhakikisha kwamba linawakamata na kuwafikisha Mahakamani baadhi ya wakazi wa kijiji cha Mbati ambao wanaojihusisha na utengenezaji na uuzaji wa pombe haramu aina ya gongo.

Pia ametoa siku tatu kwa serikali ya kijiji hicho viongozi wake kwenda ofisini kwake kujieleza kwa nini wasichukuliwe hatua za kinidhamu kutokana na kuwepo kwa wanananchi, wanaovunja sheria za nchi hivyo kukwamisha juhudi za serikali katika kupambana na vitendo vya uhalifu ambavyo vinachangia kupoteza nguvu kazi ya taifa.

Homera alitoa agizo hilo mwishoni mwa wiki, wakati alipokuwa akizungumza katika mkutano wa hadhara ambapo aliwataka wakazi wa kijiji hicho kuwafichua wale wote ambao wamekuwa kikwazo katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali, ikiwemo kazi ya ufyatuaji tofali 100,000 kwa kila kijiji agizo ambalo lilitolewa na Rais Dkt. John Magufuli.


Kadhalika kumekuwa na mgogoro wa muda mrefu wa kugombea ardhi kati ya kijiji hicho cha Mbati na kijiji jirani cha Mdabwa ambao umekuwa ukisababishwa na baadhi ya wakazi wa kijiji cha Mbati kutokana na muda mwingi hujihusisha na matumizi ya unywaji wa pombe ya gongo na kushindwa kuzuia hisia zao pale wanapokunywa jambo ambalo linachangia kuchelewesha maendeleo katika vijiji hivyo vyote viwili.

Kutokana na hali hiyo Mkuu huyo wa wilaya amewaagiza viongozi wa vijiji hivyo kwenda ofisi ya halmashauri ya wilaya hiyo kupitia idara yake ya ardhi, kumaliza suala hilo la migogoro ya mipaka ya ardhi ambalo linachangia wananchi washindwe kufanya shughuli zao za maendeleo.

Katika hatua nyingine Ofisa mtendaji wa kijiji cha Mbati Halid Maridad, anatuhumiwa kutafuna fedha shilingi milioni 1.5 ambazo zilichangwa na wakazi wa kijiji hicho kwa ajili ya utengenezaji wa madawati.

Kijiji hicho ni kati ya vijiji vitatu vinavyounda kata ya Mbati ambavyo bado vipo nyuma kimaendeleo ikilinganishwa na vijiji vingine katika wilaya ya Tunduru.

Ofisa mtendaji huyo  anadaiwa kutokomea kusikojulikana baada ya kusikia kwamba Mkuu wa wilaya, Homera na Kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo inakwenda  kijijini hapo  kwa ajili ya kupata taarifa kamili juu tukio hilo.


Homera ametao siku tatu kwa Ofisa mtendaji huyo kujisalimisha ofisini kwake popote pale alipo ili aweze kutoa ufafanuzi juu ya matumizi ya fedha hizo ambazo zilikusudiwa kukamilisha utengenezaji wa madawati ya kukalia wanafunzi.

No comments: