Friday, November 4, 2016

WATATU WASHIKILIWA POLISI WAKIDAIWA KUTOA KIPIGO NA KUSABABISHA KIFO

Na Kassian Nyandindi,            
Songea.

WATU watatu wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Ruvuma kwa tuhuma ya kuwashushia kipigo kikali watu wawili sehemu mbalimbali za miili yao, wakituhumiwa kuiba kwenye nyumba ya kulala wageni ya Jordan River iliyopo mtaa wa Majengo, Manispaa ya Songea mkoani hapa na kumsababishia kifo Anold James mkazi wa Njombe mjini mkoani Njombe.

Zubery Mwombeji.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Ofisini kwake, Kamanda  wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma Zubery Mwombeji alisema kuwa tukio hilo lilitokea Novemba 2 mwaka huu majira ya saa 12:40 asubuhi kwenye maeneo ya nyumba hiyo ya kulala wageni mjini humo.

Mwombeji alifafanua kuwa inadaiwa siku moja kabla ya tukio hilo kutokea watu wawili Anold James (25), James Exavery (18) wote wakazi wa Njombe walifika kwenye nyumba hiyo ya kulala wageni na kuomba chumba cha kulala na kwamba kwenye kitabu cha wageni aliandikishwa mtu mmoja tu ambaye ni, Anold James kisha baadaye James Exavery aliondoka akabaki Anold.

Alisema kuwa baadaye ilipofika majira ya saa za usiku kwenye chumba hicho alichokuwa amelala Anold, kulisikika sauti kuwa kuna watu wengi ndipo Meneja wa nyumba hiyo ya wageni Barnaba Said (22) alilazimika kwenda kuwachungulia ambapo aliona wamekaa kwenye chumba hicho, huku wakinywa pombe na baada ya muda mchache aligundua kuwa kunamali imeibiwa.


Said alieleza kuwa baada ya kugundua pia kaunta yake ya bar iliyopo katika eneo hilo imeibiwa alimtaarifu mhudumu wa nyumba ya kulala wageni kuwa, hata kwenye bar pia watu wasiofahamika wamevunja kaunta na kuiba na akamweleza kuwa kwenye chumba alichopanga Anold anahisi kuwa kunawatu ndipo walipoanza kumtaka Anold afungue mlango wa chumba chake, ambapo baadaye kelele zilianza kusikika kwa majirani na umati mkubwa wa watu ulifika kwenye eneo hilo huku ukimtaka Anold afungue chumba hicho.

Kamanda Mwombeji alieleza kuwa Anold alipofungua tu mlango wa chumba chake ghafla kundi la watu wenye hasira kali waliwavamia watu waliokuwemo kwenye chumba hicho na kuanza kuwashambulia kwa kuwapiga sehemu mbalimbali ya miili yao, wakiwatuhumu kuwa ni wezi ambao wameiba kwenye nyumba hiyo ya kulala wageni.

Vilevile katika tukio hilo kundi kubwa la watu walikuwa wameizunguka nyumba hiyo ya kulala wageni huku baadhi ya watu wakilazimika kutoa taarifa kituo kikuu cha Polisi Songea mjini, ambapo askari Polisi walipowasili kwenye eneo la tukio waliukuta umati huo mkubwa wa watu ambao walipoona Polisi walianza kukimbia na kutokomea kusikojulikana na kuwakuta watu wawili waliokuwa wameshushiwa kipigo wakiwa mahututi.

Kamanda huyo aliongeza kuwa hatua ya kwanza waliwachukua majeruhi hao na kuwakimbiza katika hospitali ya mkoa wa Ruvuma, ambako baada ya muda mfupi Anold James alifariki dunia wakati akipatiwa matibabu na James Exavery amelazwa na hali yake ni mbaya.


Pamoja na mambo mengine kufuatia kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa Polisi mkoani hapa, ametoa mwito kwa wananchi kutochukua sheria mkononi pale wanapowakamata watuhumiwa wa uhalifu na badala yake wanapaswa wawafikishe kwenye vyombo vya sheria ili hatua husika za kisheria ziweze kutekelezwa.

No comments: