Sunday, November 6, 2016

MBINGA WAONYWA TABIA YA KUWAFUNGIA WATOTO WENYE ULEMAVU NDANI YA NYUMBA ZAO

Baadhi ya watoto wenye ulemavu (Albino) wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa halmashauri ya mji wa Mbinga.
Na Kassian Nyandindi,               
Mbinga.

WANANCHI wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wamesisitizwa kuacha tabia ya kuwafungia ndani ya nyumba zao watoto wenye ulemavu wa aina mbalimbali badala yake wajenge mazoea ya kuwafichua watu wenye tabia ya kuwaficha watoto hao, ili waweze kupata haki zao za msingi.

Aidha wameshauriwa kuacha vitendo vya ukatili dhidi ya watu wenye walemavu ikiwemo unyanyasaji, ubaguzi na kwamba wanapaswa kujenga mazoea ya kuwapenda, kuwajali na kuwahudumia ipasavyo kama walivyokuwa watu wengine ambao hawana matatizo ya viungo.

Diwani wa viti maalumu kata ya Ruanda, Imakulatha Mapunda alisema hayo juzi alipokuwa akifungua mafunzo ya siku mbili ya sheria ya watu wenye ulemavu, yaliyofanyika katika kata hiyo wilaya ya Mbinga mkoani hapa ambayo yalifadhiliwa na shirika lisilokuwa la serikali la The Foundation for Civil Society.


“Ndugu zangu tunapaswa kuwa wasikilizaji wazuri katika mafunzo haya, huko tuendako tukayatumie vyema kwa kuyafikisha kwa wengine ambao hawakubahatika kuhudhuria hapa ili waweze kutambua haki zao za msingi”, alisisitiza Mapunda.

Naye Henry Digongwa ambaye ni mwezeshaji wa mafunzo hayo kutoka idara ya maendeleo ya jamii wilayani humo alifafanua kuwa, mambo yanayokwamisha kutotekelezeka kwa haki za watu wenye ulemavu ni pamoja na Rais wa Jamhuri ya  Muungano wa Tanzania kutoteua Mwenyekiti wa taifa wa baraza la watu wenye walemavu, ambaye angeweza kusimamia masuala mbalimbali ya kundi hilo tete.

Digongwa alifafanua pia vikwazo vingine vinavyorudisha nyuma maendeleo ya watu hao ni kutoteuliwa kwa Waziri mwenye dhamana na Wajumbe watakaowakilisha watu wenye ulemavu, katika baraza la walemavu taifa na serikali kuwa na mifumo ya kutenga bajeti ndogo ya kuhudumia watu hao ambayo haikidhi mahitaji husika.

Pia aliongeza kuwa inapaswa kuunda Kamati ndogo za kuhudumia walemavu kutoka ngazi ya mtaa, wilaya, mkoa mpaka taifa ambayo itasimamiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).

Vilevile Amos Komba ambaye ni Hakimu wa Mahakama ya mwanzo wilaya ya Mbinga, alisisitiza kuwa mlemavu yeyote yule anatafsiriwa kuwa ni binadamu mwenye haki sawa kama walivyokuwa watu wengine ambao hawana ulemavu hivyo anastahili kupata haki zote za msingi kama watu wengine.


Komba alisema kuwa pale watoto wenye ulemavu wanaponyanyaswa kwa namna moja au nyingine, mtu yeyote sheria inamruhusu kutoa malalamiko kwa Kamati ya maofisa wa ustawi wa jamii au kwenda kushtaki Mahakamani kufungua mashtaka dhidi ya kosa aliloliona linafanyika.

No comments: