Sunday, February 12, 2017

DC AWAPONGEZA MADIWANI MBINGA

Na Kassian Nyandindi,    
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Cosmas Nshenye amewapongeza wajumbe wa kikao cha maridhiano ya kugawana mali kati ya pande mbili za halmashauri ya mji wa Mbinga na wilaya ya Mbinga kwa kumaliza kikao hicho katika hali ya amani, utulivu na maelewano bila ya kuwepo kwa mgogoro, mvutano na malumbano.

Cosmas Nshenye.
Nshenye ambaye alikuwa Mwenyekiti wa kikao hicho, alitoa pongezi hizo juzi wakati alipokuwa akizungumza na Madiwani wa halmashauri hizo katika kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo mjini hapa.

Alisema kuwa kitendo hicho kimeonyesha utashi na ukomavu wa kifikra kwa kile alichoeleza kuwa kuna baadhi ya maeneo mengine wanapokuwa kwenye vikao kama hivyo, imekuwa ikizuka migogoro na malumbano ambayo yanachangia kwa kiasi kikubwa kukwamisha shughuli za maendeleo ya wananchi huku akisisitiza kuwa uhamisho wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga utafanyika mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa ofisi zao.

Akichangia hoja kwenye kikao hicho, Mwenyekiti wa halmashauri ya mji wa Mbinga Kipwele Ndunguru alisema kuwa mapendekezo yaliyoridhiwa na kikao cha kamati ya ushauri ni kuhamisha bajeti ya shilingi bilioni 2.1 ambayo ilikuwa inatakiwa kujenga boma la halmashauri hiyo na kuzihamishia halmashauri ya wilaya ya Mbinga ambapo mpaka sasa kwa kuanzia kimetolewa kiasi cha shilingi milioni 500.


Naye Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Ambrose Nchimbi alisema kuwa kwa upande wa baraza la Madiwani wa halmashauri hiyo pia wameridhia kutoa mali zote zisizohamishika na kuzikabidhi kwa halmashauri ya mji wa Mbinga.

Aidha Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga Gombo Samandito, alisema kuwa haoni sababu ya kulumbana na kuvutana kwa sababu ya kugombea mali kwa madai kuwa halmashauri zote mbili zipo kwa ajili ya kuitumikia serikali moja na wananchi wake, ambapo hoja hiyo iliungwa mkono na Madiwani wa pande zote huku mmoja wa madiwani hao Benedict Ngwenya akidai kuwa maendeleo yoyote yanapatikana pale mahali ambapo kunakuwa na upendo na maelewano.


Kwa upande wake Mbunge wa jimbo la Mbinga mjini, Sixtus Mapunda alipongeza jitihada zilizofanyika kwa kumaliza suala hilo kwa maelewano mazuri katika kushughulikia suala la mgawanyo wa mali jambo ambalo alidai kuwa awali lilikuwa linakwamisha kufanya shughuli za maendeleo huku Mkurugenzi wake mtendaji wa halmashauri hiyo, Robert Mageni akiwaomba Madiwani wa halmashauri ya mji huo kuendelea kujenga umoja na mshikamano.

No comments: