Saturday, February 11, 2017

DC: VITUO VYA KUTOLEA HUDUMA YA AFYA MBINGA KUMEKUWA NA TATIZO LA UKOSEFU WA DAWA

Sehemu ya watumishi wa halmashauri ya wilaya Mbinga, wakimsikiliza Mkuu wa wilaya hiyo Cosmas Nshenye.
Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Cosmas Nshenye amesema kuwa katika wilaya hiyo kumekuwa na malalamiko mengi kutoka kwa wananchi ambayo amekuwa akiyapokea kwa nyakati tofauti kwamba katika vituo vya kutolea huduma za afya wilayani humo, kumekuwa na tatizo la ukosefu wa dawa jambo ambalo limekuwa ni kero kubwa kwa wananchi.

Aidha kufuatia hali hiyo amewataka watendaji waliopewa dhamana kusimamia kikamilifu majukumu yao ya kazi ikiwemo kujipanga ipasavyo katika kuhudumia wagonjwa wanaokwenda kutibiwa ili kuweza kuondoa malalamiko hayo yasiyokuwa ya lazima.

Nshenye alisema kuwa tatizo hilo linaanzia hospitali ya wilaya ambapo malalamiko juu ya ukosefu wa dawa yamekuwa yakitolewa na wananchi kwa muda mrefu na kwamba wamekuwa wakilazimika wakati mwingine kwenda kununua dawa hizo kwenye maduka ya dawa muhimu badala ya kupewa hospitalini hapo.


Mkuu huyo wa wilaya ya Mbinga, Nshenye alisema hayo juzi wakati alipokuwa akihutubia katika baraza la Madiwani wa halmashauri ya mji wa Mbinga ambalo lilifanyika kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo mjini hapa.

“Nawaombeni sana tusimamie kikamilifu suala la dawa katika maeneo yetu ya kutolea huduma za afya, mimi nisingependa kusikia hili tunapaswa kuwahudumia wagonjwa wetu ili waweze kupata matibabu kwa ufasaha”, alisisitiza Nshenye.

Pia alisema kuwa anachukizwa na tabia kwa baadhi ya Waganga wafawaidhi kutokuwepo masaa ya kazi katika vituo vyao vya kutolea huduma za afya, hivyo amekemea tabia hiyo na kuwataka waache mara moja na badala yake wakae katika vituo hivyo ili waweze kuhudumia wagonjwa.


Hata hivyo aliongeza kuwa hali hii inaonesha kwamba watendaji hao wa serikali hawajajipanga vizuri katika kuhudumia wananchi na kwamba ofisi yake iwe ni mwisho kusikia au kuona maeneo ya kutolea huduma za afya kwamba hayana dawa.

No comments: