Tuesday, February 28, 2017

GOMBO SAMANDITO AWAKEMEA WALIMU WATORO KAZINI ASISITIZA ATAKAYEKAMATWA ATAMFUKUZA KAZI

Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

WALIMU wa shule za msingi na sekondari katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wametakiwa kuzingatia maadili ya kazi zao ikiwemo kuacha vitendo vya ulevi na utoro kazini.

Aidha wamesisitizwa kuwahi na kuwa katika mazingira ya kazi wakati wote na kufuata taratibu za kazi zao kwa mujibu wa nafasi walizonazo kazini.

Gombo Samandito.
Hayo yalisemwa na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Gombo Samandito wakati alipokuwa akizungumza kwenye kikao cha tathimini ya maendeleo ya elimu kilichofanyika kwenye ukumbi wa Kanisa Katoliki Jimbo la Mbinga mjini hapa.

“Walimu mnatabia ya kuwa watoro kazini natambua mnajua kwamba zikipita siku tano haupo kazini nakufukuza kazi, wakati wa kazi fanyeni kazi zenu kwa kutekeleza ipasavyo majukumu mliyopewa mkayasimamie haya vizuri msiwe sehemu ya matatizo”, alisisitiza Samandito.


Samandito alisisitiza pia kwa atakayepuuza maagizo yake hatua kali za kinidhamu zitachukuliwa dhidi yake ikiwemo kufukuzwa kazi huku akiongeza kuwa adui mkubwa wa maendeleo katika maisha ya kila siku ya binadamu ni tabia ya mtu husika hivyo walimu hao wanapaswa kujiangalia kwanza wenyewe na kubadilika mara moja kuwa na tabia nzuri kazini.


Vilevile amekemea tabia ya walimu kukopa hovyo kwenye taasisi za kifedha kupita kiasi jambo ambalo alieleza kuwa ni kinyume na taratibu husika, hivyo wakope kwa kufuata taratibu zilizowekwa na sio vinginevyo.

“Walimu jaribuni kuliangalia hili haya mambo yaangalieni sana ole wake nitakayemkamata atakiona cha mtemakuni, hiyo huruma ya msamaha sina kabisa nitakuchukulia hatua za kinidhamu pale nitakapokuona umekiuka maagizo haya ikiwemo kukufukuza kazi”, alisisitiza.

Kwa upande wao wakichangia hoja katika kikao hicho cha Wadau wa elimu kwa nyakati tofauti, Magnus Mpokwa ambaye ni mzee maarufu kutoka kata ya Mkako wilayani Mbinga alisema kuwa maofisa elimu kutoka ngazi ya kata hadi wilaya wanapaswa sasa kuacha kukaa maofisini badala yake waondoke na kwenda vijijini kukagua maendeleo kwa shule za msingi na sekondari.


Hata hivyo naye Mario Kitusi ambaye ni mwalimu Mkuu shule ya msingi Mahumbato wilayani humo alisisitiza kuwa ili elimu iende vizuri ni lazima kuwepo na mshikamano kati ya wazazi, walimu na viongozi wengine wote na kwamba serikali inapaswa pia kuboresha maslahi ya elimu ili taaluma iweze kusonga mbele.

No comments: