Sunday, February 5, 2017

MPANGO WA KUUZA KAHAWA KWA JINA LA EX MBINGA WANUFAISHA WAKULIMA

Upande wa kushoto ni mtaalamu wa mimea na udongo Kaminyoge Mhamerd akiwa katika eneo la shamba darasa la kilimo cha kahawa, kikundi cha Unango kata ya Ngima wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma akiwaelimisha wakulima wa zao hilo wazingatie kanuni bora za kilimo cha zao hilo.
Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

KATIKA kuhakikisha kwamba wananchi wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wanaendelea kunufaika na uzalishaji wa zao la kahawa wilayani humo, wilaya inaendelea kutekeleza mpango wa kuhifadhi na kuuza kahawa ikiwa na jina la Ex Mbinga, badala ya Miji ya Makambako mkoani Njombe kama ilivyokuwa hapo awali.

Aidha mpango huo wa kuuza kahawa kwa majina ya Ex Makambako ulikuwa ukisababisha kupunguza faida ya mauzo ya kahawa kwa mkulima na kuhamasisha wafanyabiashara kutorosha kahawa ya Mbinga na kumfanya mkulima aendelee kupata hasara.

Taarifa hiyo ilitolewa na Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Cosmas Nshenye ambapo alifafanua kuwa gharama hizo kwa mkulima hivi sasa zimepungua ikiwemo na suala la utoroshaji wa kahawa, hali ambayo inavutia hata kuwepo kwa wawekezaji wa zao hilo wilayani humo.


Vilevile akizungumzia juu ya mwenendo wa uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara, Nshenye alisema kuwa kiwango cha uzalishaji wa mazao hayo kimeongezeka kutokana na mikakati mbalimbali iliyowekwa na kutekelezwa ikiwemo kuongezeka kwa matumizi ya mbegu bora, uhamasishaji wa kilimo cha kahawa, korosho na zao la mpunga uliofanywa na wilaya kwa kushirikiana na wadau wa kilimo.

Nshenye aliongeza kuwa kutolewa kwa elimu ya ugani kwa wakulima na uwepo wa pembejeo za ruzuku nao umechangia kwa kiasi kikubwa uzalishaji huo kuwa wenye tija katika jamii.

Kwa upande wa sekta ya ushirika alibainisha kuwa kazi kubwa inayofanywa hivi sasa ni kuendelea kutoa elimu kwa wananchi, waweze kujiunga na vyama vya ushirika kwa lengo la kuwa na nguvu ya pamoja katika kukabiliana na changamoto mbalimbali za kukuza uchumi wao.

Mkuu huyo wa wilaya alisema kuwa wilaya ya Mbinga ina jumla ya vyama vya ushirika 63 vyenye wanachama 13,716 ambapo vya akiba na mikopo yaani SACCOS navyo vipo 34 vyenye wanachama 33,757 wenye jumla ya hisa shilingi milioni 184,598,800.


Kadhalika alieleza kuwa mikopo iliyotolewa mpaka sasa katika vyama hivyo ina jumla ya shilingi bilioni 8,220,702,457 na kwamba sehemu ya mikopo iliyorejeshwa ni shilingi bilioni 4,394,414,162 hivyo bado kurejeshwa mikopo ya shilingi bilioni 3,826,288,295.

No comments: