Sunday, February 26, 2017

SONGEA WAPONGEZWA KWA KUKUZA TAALUMA ELIMU YA MSINGI NA SEKONDARI

Na Kassian Nyandindi,     
Songea.

POLOLET Kamando Mgema, ambaye ni Mkuu wa wilaya ya Songea mkoani Ruvuma amewapongeza walimu wa shule za msingi na sekondari katika Manispaa ya Songea mkoani humo, kwa kufanya kazi nzuri ambayo imeleta mafanikio mazuri ya kukuza taaluma katika matokeo ya mitihani darasa la saba na kidato cha nne.

Mkuu huyo wa wilaya alitoa pongezi hizo kwenye kikao cha tathimini ya elimu kwa mwaka wa 2015/2016 ambacho kiliwakutanisha Wadau mbalimbali wa elimu Waratibu elimu kata, Walimu wakuu wa shule za msingi, Wakuu wa shule za sekondari, Madiwani na Maofisa elimu ambacho kilifanyika kwenye ukumbi wa shule ya sekondari ya wasichana Songea.       

Pamoja na kuwapatia pongezi hizo, Mgema alikemea pia tabia zinazofanywa na baadhi ya walimu kuwa na utoro kazini ambapo amewataka waache mara moja vinginevyo kwa yule atakayebainika hatua kali za kisheria zitachukuliwa ikiwemo kufukuzwa kazi.


Kwa upande wake Ofisa elimu sekondari Manispaa ya Songea Devotha Luongo alisema kuwa hatakubaliana na vitendo vitakavyofanywa na mwalimu yeyote ambaye ataonesha udhaifu kwenye maeneo yake ya kazi kwa mambo ya ulevi na utoro kazini vinginevyo ajiondoe mwenyewe mapema.

Luongo alisema kuwa amefurahishwa na matokeo ya mitihani ya kidato cha nne katika kipindi cha mwaka jana ambapo wanafunzi walioshika nafasi za kwanza kimkoa kwenye mtihani wa Fizikia na Mtihani wa Kemia walitoka shule za sekondari za Manispaa ya Songea, hivyo ni vyema Wadau wa elimu wakiwemo wazazi wanapaswa kuendelea kuwahimiza watoto wao kusoma kwa bidii na sio kuwaacha mitaani wakizurula.

Editha Kagomba ambaye naye ni Ofisa elimu kwa shule za msingi katika Manispaa hiyo alisema kuwa asilimia 55 ya wanafunzi wa shule hizo wamekuwa wakihudhuria masomo darasani lakini kumekuwa na wale ambao ni watoro hawahudhurii masomo hayo ambapo wamefikia asilimia 45.


Aliwataka Walimu wakuu kwa shule za msingi pamoja na Waratibu elimu kata kuona umuhimu wa kuhimiza wazazi kujenga mahusiano mazuri kati yao na walimu kwa lengo la kuhakikisha watoto wote wanakwenda shule na kwamba ameiomba serikali kuendelea kuajiri walimu katika shule hizo ili kuweza kupunguza tatizo la uhaba wa walimu lililopo sasa.

No comments: