Wednesday, February 8, 2017

SAMANDITO: MPANGO WA BAJETI MBINGA UNALENGA KUBORESHA HUDUMA ZA KIJAMII NA KUKUZA UCHUMI KWA KUZINGATIA DIRA YA MAENDELEO YA TAIFA KUWA NA VIWANDA VYA KATI

Aliyesimama ni Mkurugenzi mtendaji Halmashauri wilaya ya Mbinga, Gombo Samandito akitoa ufafanuzi juu ya mambo mbalimbali katika kikao cha Bajeti baraza la Madiwani wilayani humo kilichoketi leo mjini hapa. Katikati ni Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Ambrose Nchimbi na Makamu mwenyekiti Benward Komba.

Na Kassian Nyandindi,    
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa malengo makuu ya mpango wa bajeti kwa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma ni kuimarisha amani na utawala bora, kuboresha huduma za kijamii, kukuza uchumi wa wilaya hiyo kwa lengo la kuboresha maisha ya wananchi wake, sambamba na dira ya maendeleo ya taifa inayolenga Tanzania kuwa nchi ya viwanda vya kati.

Aidha halmashauri hiyo inaendelea na jitihada za kuongeza vyanzo vipya vya mapato ya ndani badala ya kutegemea zao la kahawa pekee ambalo hivi sasa halikidhi mahitaji husika, ambapo jitihada zinafanyika za kutafuta wawekezaji watakaoweza kutumia rasilimali zilizopo wilayani humo kama vile madini, ardhi na misitu viweze kuingiza mapato zaidi.

Hayo yalisemwa na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Gombo Samandito wakati alipokuwa akitoa maelezo mafupi juu ya rasimu ya mpango wa bajeti kwa Baraza maalum la Madiwani wa halmashauri hiyo, mwaka wa fedha 2017 hadi 2018 lililoketi leo kwenye ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa.

Samandito alisema kuwa kuongezeka kwa fedha hizo za mapato kutatokana pia na fedha za upimaji wa mashamba ya kahawa ambapo ekari moja hupimwa kwa shilingi 100,000 na kwamba tayari mashamba 70,000 ya wananchi wilayani humo yamepimwa na wahusika kupewa hati za kimila huku halmashauri ikiweza kupata shilingi bilioni 7,000,000,000.


Kadhalika aliongeza kuwa tayari viwanja 125,000 vimepimwa katika miji midogo mbalimbali iliyopo wilayani hapa ambavyo vinatarajia kuiingizia halmashauri shilingi bilioni 2,500,000,000 ambapo utekelezaji huu ni wa sera ya taifa ya ardhi na mpango wa pili wa maendeleo ya taifa wa miaka mitano unaotaka kila kipande cha ardhi kipimwe hapa nchini.

Afisa mipango wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Onesmo Mapunda akiwasilisha bajeti ya mpango huo wa fedha kwa Baraza hilo la Madiwani, alisema kuwa bajeti ambayo wanatarajia kuitumia katika kipindi hicho ni ya shilingi bilioni 46,591,949,782 ambapo kati ya hizo shilingi bilioni 27,394,490,248 ni mishahara ya wafanyakazi, shilingi bilioni 1,809,347,616 ni kwa ajili ya matumizi mengineyo.

Pia katika bajeti hiyo shilingi bilioni 7,830,382,900 zitatumika kwa ajili ya miradi ya maendeleo ya wananchi na kwamba mapato ya ndani yamekadiriwa kukusanywa kufikia shilingi bilioni 9,557,729,018.  

Bajeti hiyo ilipitishwa katika kikao hicho ambacho kilikuwa kikiongozwa na Mwenyekiti wake, Ambrose Nchimbi na kuhudhuriwa na wakuu wa idara pamoja na watendaji wa kata wa wilaya hiyo na kueleza kuwa imezingatia makubaliano waliyoketi katika vikao vya kamati mbalimbali.

Nchimbi alisisitiza kuwa vipaumbele vya bajeti hiyo ni kukamilisha miradi ya miaka ya nyuma ambayo ilikuwa bado haijakamilika ujenzi wake, pamoja na kuongeza vyanzo vipya vya mapato ya ndani badala ya kutegemea zao la kahawa pekee ambalo hivi sasa halikidhi mahitaji husika ya halmashauri.

Aliongeza kuwa bajeti hiyo pia imelenga kuboresha ujenzi wa miundombinu ya elimu katika shule za msingi na sekondari, kuboresha huduma za afya kwa kukamilisha ujenzi wa zahanati, kutengeneza madawati na viti kwa ajili ya shule za msingi na sekondari, ujenzi wa nyumba za watumishi katika shule za msingi na sekondari, kuboresha mtandao wa barabara za halmashauri, pamoja na kuandaa mpango mkakati mpya wa maendeleo ya wananchi na halmashauri kwa ujumla.

Kwa upande wake Mwenyekiti huyo wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Nchimbi amewapongeza pia Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo Samandito na Afisa mipango Mapunda pamoja na timu nzima ya wataalamu kwa kuandaa vizuri taarifa ya bajeti na mpango wa maendeleo ya wananchi wa wilaya hiyo, kwa mwaka wa fedha wa 2017/2018 ambapo amedai kuwa endapo itapitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaweza kuleta sura nzuri ya mafanikio makubwa kwenye upande wa miradi ya maendeleo.

No comments: