Tuesday, January 8, 2013

WATOTO MKOANI RUVUMA KUPATIWA CHANJO YA VICHOMI NA KUHARISHA

Na Steven Augustino,
Songea.

ZAIDI ya watoto 53,000 wenye umri chini ya miaka mitano mkoani Ruvuma, wanatarajiwa kupata chanjo mpya ya ugonjwa wa kichomi na kuharisha mkoani humo.

Wakati taarifa za takwimu za magonjwa hayo zikitolewa, zinaonesha  kusababisha watoto takribani 6000 kupoteza maisha kila mwaka na kushika nafasi ya pili na ya tatu kwa kusababisha vifo vingi vya watoto yakitanguliwa na ugonjwa wa Malaria.

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Mwambungu alisema hayo wakati wa uzinduzi wa chanjo hizo za kuzuia ugonjwa wa kichomi na kuharisha, kwa watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano ambao umekuwa ukisababisha vifo vingi kwa watoto hao.


Akizungumza katika uzinduzi wa chanjo hiyo mpya mkuu huyo wa mkoa aliwaonya watu wanaowatisha akina mama ili wasiwapeleke watoto wao kupata chanjo, kuacha vitisho hivyo mara moja na atakayebainika atachukuliwa hatua za kiisheria.

Aidha katika tukio hilo Mwambungu, aliweza kuzindua kwa kuwapa watoto matone ya dawa hizo za chanjo ambao walifikishwa katika hospitali ya mkoa mjini Songea.

Na mkuu huyo wa mkoa alipomaliza zoezi hilo aliwahimiza akina mama wenye watoto kuwapeleka katika vituo vya tiba ili wapate chanjo hiyo mapema na wasikubali kurubuniwa au kudanganywa juu ya tiba za dawa hizo.

Awali mganga mkuu wa mkoa wa Ruvuma Dkt. Daniel Malekela  alimueleza mkuu huyo wa mkoa kwamba maandalizi ya kutoa chanjo hiyo katika mkoa huo yamekamilika na kwamba chanjo hiyo ni salama.

Dkt.  Malekela alisema kuwa Chanzo hizo ni salama na zimethibitiswa na Shirika la Afya Duniani(WHO) kuwa hazina madhara.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti  baada ya kukamilika kwa uzinduzi wa chanjo hiyo, baadhi ya akina mama walisema wamepokea kwa mikono miwili na kuwataka wenzao wajitokeze kwa kuwataka watoto wao wapewe  matone hayo ili wasishambuliwe na magonjwa ya kichomi na kuharisha.

No comments: