Friday, May 17, 2013

ASKOFU MTEGA AELEZA SABABU ZA KUJIUZURU

Askofu Norbeth Mtega.





































Na Mwandishi Maalum,
Songea.

ASKOFU Mkuu wa Kanisa Katoriki, Jimbo Kuu la Songea, mkoani Ruvuma ambaye juzi ametangaza kujiuzulu, Norbert Mtega, ameelezea sababu zilizomfanya achukue uamuzi huo.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, alisema hali hiyo inatokana na kusumbuliwa na magonjwa mbalimbali ambayo ni presha, miguu, magoti kujaa maji na kukosa usingizi kwa muda mrefu hivyo kujisikia kizunguzungu na tayari amewahi kuanguka zaidi ya mara nne.

Alisema jamii inayomtazama inamuona yupo kawaida lakini ana matatizo makubwa ya kiafya kwa muda mrefu ila alikuwa akijitahidi kufanya kazi za kitume hali ambayo imechangia afya yake kuendelea
kuwa dhoofu.


Aliongeza kuwa, tatizo la afya yake ni la muda mrefu hivyo ni bora astaafu mapema kabla ya kupoteza kumbukumbu ili aweze kumpa Baba Mtakatifu muda wa kutafuta Askofu mwingine ambaye ataweza kuongoza jimbo hilo.

“Nimeamua kujiuzulu kwa manufaa ya Wakatoliki wote, Jimbo Kuu la Songea na jamii kwa ujumla ili niweze kupatiwa matibabu kwani nikiendelea kung’ang’ania uongozi, hasara yake ni kubwa sana kwa jamii ninayoiongoza.

“Namuomba Mungu anipe afya njema ili niweze kutoa ushauri zaidi kwa waumini, Mapadri na Serikali,” alisema.

Amewahimiza waumini na viongozi wa dini, kuendelea kuwa na ushirikiano, kuacha tofauti za ukabila ambazo zinachangia kurudisha nyuma maendeleo ya Mkoa huo kwani ukabila ni hatari na unaweza kuwagawa, kukwamisha maendeleo.

Alisema yeye anatambua kuwa, watu wengi wameshtuka kutokana na uamuzi aliochukua hasa kwa kuzingatia kuwa, alikuwa akifanya kazi zake bila wasiwasi.

Amemtaka Askofu ajaye, kuhakikisha anaendeleza mema aliyoanzisha hususani katika nyanja ya elimu, afya, maji, mazingira ili kuwaletea wananchi maendeleo na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano na ushauri.

Mkazi wa Mkoa huo, Watson Nganiwa, alisema Mtega atakumbukwa kutokana na kuwajengea uwezo wananchi wajitegemee na kuacha kutegemea wafadhili, kuhimiza wafanye kazi kwa bidii si kutegemea misaada.

Alikuwa akishiriki shughuli mbalimbali za kijamii, kiserikali na kuwashirikisha viongozi wa Serikali pamoja na kukemea maovu miongoni mwa jamii bila woga.

Wananchi wengi wamempongeza kwa uamuzi aliochukua na kumtakia afya njema ili aweze kupona, kuendelea kutoa ushauri na kuwataka viongozi wengine kuiga mfano wake.

Mtega amelitumikia Jimbo la Iringa kwa miaka sita na baadaye Jimbo la Songea miaka 22 hivyo amekuwa askofu kwa muda wa miaka 28, Kiongozi wa Idara ya Elimu katika Baraza Kuu la Maaskofu na Msimamizi wa kitume katika majimbo nane.

No comments: