Thursday, May 2, 2013

TUNDURU SEKTA YA ELIMU BADO KUNA MATATIZO


Na Steven Augustino,
Tunduru.

MADIWANI wameiomba Serikali kuwabana baadhi ya walimu wa shule za Msingi na Sekondari, wanaoendesha miradi ya kuonesha picha za video katika maeneo ya shule, huku wakieleza kuwa ni miongoni mwa vikwazo vya maendeleo ya elimu kwa watoto wao.

Hayo yalisemwa na diwani wa viti maalum katika kata ya Nalasi Alus Yunusi, ambaye alisema kutokana na hali hiyo walimu hao wamekuwa hawazingatii maendeleo ya taaluma kwa wanafunzi, zaidi ya kuangalia maslahi yao yatokanayo na miradi hiyo.

Akifafaa taarifa hiyo Yunusi alisema kuwa hayo ameyabaini katika tarafa yake, ambapo biashara hiyo ya kuonyesha picha za video imekithiri na kwamba endapo watafumbiwa macho taaluma katika wilaya hiyo itaendelea kuporomoka.

Kufuatia hali hiyo Diwani huyo akatumia nafasi hiyo kuwakumbusha wakaguzi wa shule, kutazama changamoto hiyo na kuweka mikakati ya kuidhibiti na ikiwezekana biashara hiyo izuiliwe kufanyika katika maeneo ya shule.

Alisema kutokana na hali hiyo walimu hao wamekuwa hawawezi kuwakemea wanafunzi hao, hata wakifanya matukio mabaya kwa vile wao ndio wateja wakubwa wa kuangalia picha za video.

Diwani wa kata ya Masonya Fadhili Mshamu  na diwani wa viti maalumu katika tarafa ya Nampungu  Sikudhani Chikambo, walieleza kilio cha ukosefu wa nyumba za walimu katika shule za wilaya ya Tunduru, huku wakisisitiza ni vyema  iwekwe mikakati ya kumaliza tatizo hilo ili walimu waondokane na adha ya kupanga uswahilini.

Diwani Chikambo katika taarifa yake pia alieleza kilio cha utoro wa kupindukia  katika shule ya msingi Mchekeni, ambapo alisema kuwa hivi sasa kuna darasa moja wanasoma wanafunzi wawili tu, hali ambayo alisema inahitaji mikakati ya makusudi kuwaokoa watoto wao kwa kuwafanya wapende masomo.

Aidha taarifa ya madiwani hao pia ikabainisha ubovu wa miundo mbinu ya shule pamoja na uchakavu wa madarasa katika shule  nyingi wilayani humo,   kutokana na kuta zake kubomoka.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Tunduru Robert Nehatta alisema kuwa, halmashauri yake imejipanga kuhakikisha kuwa inaboresha miundombinu katika maeneo ya kazi, ikiwemo ujenzi wa nyumba za walimu na miradi mingine ya maendeleo ya wananchi.

No comments: