Monday, May 27, 2013

VIONGOZI CHADEMA MBINGA WAFUNGASHA VIRAGO, KUTOKANA NA KUTOWAJIBIKA IPASAVYO

Freeman Mbowe.
























Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.


HALI ya kisiasa kwa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma imeendelea kuwa tete, kufuatia viongozi wa chama hicho ngazi ya Wilaya na Jimbo kuvuliwa madaraka, kutokana na kushindwa kukiimarisha chama na kutowajibika ipasavyo.

Kauli hiyo ilitolewa na aliyekuwa Katibu wa Baraza la vijana la chama hicho (BAVICHA) Felix Katoto, ambaye hivi sasa anashikilia ofisi ya CHADEMA wilayani Mbinga kwa muda, kutokana na uongozi uliokuwa awali kuondolewa madarakani.

Katoto alisema hayo alipokuwa akihojiwa na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake, ambapo alieleza pia uongozi huo wa awali ulikuwa hautekelezi majukumu ya chama kwa mujibu wa taratibu walizojiwekea, na ndio maana wamefikia maamuzi hayo.


“Tumefanya hivi tukiwa na malengo ya kukijenga chama chetu, uongozi uliopita ulikuwa una matatizo ambayo hata yamesababisha chama kushindwa katika chaguzi mbalimbali zilizofanyika ndani ya wilaya hii”, alisema.

Alifafanua kuwa chaguzi hizo ni za nafasi ya diwani, ambazo madiwani wa maeneo husika mmoja alifariki dunia wa kata ya Langiro na mwingine aliyejiuzuru wa kata ya Mpepai ambapo wakati uchaguzi unafanyika katika maeneo hayo, aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA Desderius Haulle na viongozi wenzake, muda mwingi walikuwa wakizembea na hata wakati mwingine kuonekana wakishiriki kukidondosha chama kisiweze kushinda katika chaguzi hizo zilizofanyika hivi karibuni.

“Uwezo wa kushinda katika kata hizi tulikuwa nao kwa kiasi kikubwa lakini hawa viongozi wenzangu ambao sasa hatupo madarakani, walikuwa hawazingatii majukumu yao waliyopewa kiasi ambacho hata fomu za wagombea wetu siku ya mwisho ya kuzirejesha utakuta zinamapungufu”, alisema Katoto.

Aidha alitolea mfano kwa kata ya Langiro ambayo uchaguzi umefanyika hivi karibuni, kwamba siku wanarejesha fomu ya mgombea wao wa udiwani ilipopokelewa na msimamizi wa uchaguzi ilikuwa na mapungufu makubwa, kama vile kutogongwa mihuri na kuwekwa sahihi na wahusika na hatimaye kushindwa kuingia kwenye kinyang’anyiro hicho hivyo mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kufikia hatua ya kushinda bila kupingwa.

Kutokana na uzembe huo alisema wanachama wa CHADEMA wilayani Mbinga, walikuwa wakiutupia lawama uongozi uliokuwa madarakani hivyo baada ya malalamiko hayo kufikishwa katika ngazi husika, ndipo walipotakiwa kuwajibika kuondoka madarakani na wakati wowote uchaguzi wa viongozi wengine wapya utafanyika mara baada ya taratibu husika kukamilika.

Kadhalika alipoulizwa Mwenyekiti wa CHADEMA wa mkoa wa Ruvuma, Joseph Fuime alithibitisha kwa uongozi wa chama hicho wilaya ya Mbinga kuondolewa madarakani, huku akisema wakati uongozi huo unawajibika kutekeleza hilo yeye alishiriki kusimamia suala hilo.

Viongozi waliojiuzuru na wadhifa wao kwenye mabano ngazi ya Wilaya ni Desderius Haulle (Mwenyekiti), Alfonce Nchimbi (Katibu), Ferdinand Mbelle (Katibu Mwenezi), Gaudensia Komba (Mwenyekiti baraza la umoja wa akina mama), Anastazia Magubika (Katibu wa baraza la umoja wa akina mama), Menas Ndunguru (Mwenyekiti baraza la wazee), Nathaniel Ndunguru (Katibu baraza la wazee), Dominicus Ngalima (Mwenyekiti baraza la vijana) na Felix Katoto (Katibu baraza la vijana).

Wengine kwa ngazi ya Jimbo ni Winfrid Ndunguru (Mwenyekiti), Pius Ndimbo (Katibu), Daud Mwalongo (Katibu mwenezi), Theopista Haulle (Baraza la umoja wa akina mama), Magreth Swai (Katibu baraza la umoja wa akina mama), Peter Ngunguta (Mwenyekiti baraza la wazee), Jacob Ndunguru (Katibu baraza la wazee), Jacob Ngonyani (Mwenyekiti baraza la vijana) na Stanley Ndunguru (Katibu baraza la vijana).



No comments: