Monday, May 8, 2017

HALMASHAURI MJI WA MBINGA WATAKIWA KUENDELEZA MAPAMBANO DHIDI YA UGONJWA WA MALARIA

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa, Amour Hamad Amour akipokea zawadi ya kahawa iliyosagwa kitaalamu kutoka kwa Deogratias Haulle ambaye ni mtaalamu wa kutengeneza kinywaji hicho kutoka Kiwanda cha kukoboa kahawa Mbinga(MCCCO) mkoani Ruvuma. Hata hivyo kahawa hiyo alikabidhiwa katika eneo la banda la maonyesho kwenye mkesha wa Mwenge wa Uhuru uwanja wa Masumuni uliopo mjini hapa.
Na Kassian Nyandindi,         
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa hali ya vifo vinavyosababishwa na ugonjwa wa Malaria kwa akina mama Wajawazito, Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma katika kipindi cha mwaka 2016/2017 imefikia kuwa ni asilimia 1.9 na kwa upande wa Watoto chini ya miaka mitano ni asilimia 9.6 ambapo halmashauri hiyo inaendelea na mikakati mbalimbali ya mapambano dhidi ya kuutokomeza ugonjwa huo.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga Cosmas Nshenye alisema hayo juzi alipokuwa akisoma risala ya utii wa wananchi wa halmashauri ya mji wa Mbinga kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli ambayo ilisomwa mbele ya kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Amour Hamad Amour katika viwanja vya Masumuni mjini hapa.

Nshenye alisema kuwa mapambano hayo dhidi ya ugonjwa wa Malaria wamejipanga kikamilifu kwa kuhakikisha wanatekeleza, elimu ya Kinga dhidi ya ugonjwa huo inaendelea kutolewa kwa wananchi ambapo mpaka sasa jumla ya kata 19 na vijiji 49 vimefikishiwa elimu husika ikiwemo kufanya usafi wa mazingira na matumizi sahihi ya vyandarua.


Alisema kuwa jumla ya vyandarua 1,681 vimegawiwa kwa akina mama wajawazito na watoto waliochini ya umri wa miaka mitano ambapo huduma hiyo imekuwa ikitolewa kwa kundi hilo pale wanapohudhuria kliniki kwa mara ya kwanza.

“Halmashauri kwa kushirikiana na wadau wa ndani na nje hapa wilayani tumeendelea na kampeni maalum ya kupambana na malaria kama vile kutoa elimu, kuhamasisha kusafisha mazingira, kupima na kutoa tiba ya ugonjwa huu,

Wananchi wamekuwa wakiendelea kuhamasika katika kupambana na Malaria kwa kusafisha mazingira ya makazi, matumizi sahihi ya vyandarua na Kuzingatia huduma ya matibabu dhidi ya ugonjwa huu”, alisema Nshenye.

Pia alibainisha kuwa makundi maalum nayo yamekuwa yakishirikishwa katika kampeni na programu za kupambana na ugonjwa huo kupitia mikutano ya hadhara, matamasha au mikusanyiko maalum na sherehe za maazimisho mbalimbali.

Kwa upande wake kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Amour Hamad Amour alipongeza jitihada hizo zinazofanywa na kutaka ziendelezwe ili kuweza kufikia malengo ya kuutokomeza ugonjwa huo ambao ni hatari katika jamii.

Vilevile Amour alisema kuwa taifa lenye nguvu ni lile ambalo watu wake wana afya bora hivyo wananchi wanapaswa kuzingatia kanuni bora za afya na tiba ili kuweza kufikia nyanja bora ya kimaendeleo kwa faida ya kizazi cha sasa na kile kijacho.


No comments: