Thursday, May 25, 2017

KUFUNGWA KWA BENKI YA WANANCHI MBINGA MASWALI NI MENGI KULIKO MAJIBU

Na Kassian Nyandindi,   
Mbinga.

KUFUATIA Benki Kuu ya Tanzania (BOT) kufunga milango ya Benki ya Wananchi Mbinga (MCB) isiendelee kufanya kazi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, Mtandao wa Mashirika yasiyokuwa ya Serikali (MBINGONET) wilayani humo wamesema kuwa kufilisika kwa benki hiyo kumesababishwa na viongozi waliopewa dhamana ya kuiendesha kutokuwa makini na utendaji kazi, usimamizi na utekelezaji wa majukumu husika.

Aidha MBINGONET wameiomba BOT ifanye uchunguzi wa kina juu ya suala hilo na wahusika wachukuliwe hatua kali za kisheria ikiwemo kufikishwa Mahakamani, kwani ikumbukwe kuwa MCB ilikuwa ni mkombozi wa wakulima wadogo wadogo ikiwemo vikundi vya ujasiriamali vilivyopo ndani na nje ya wilaya hiyo.

Hayo yalisemwa na Katibu wa Mtandao huo wa mashirika yasiyokuwa ya serikali wilayani Mbinga, Benedict Luena wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa.

Luena alieleza kuwa imekuwa ni jambo la aibu kwa wanambinga kupitia vijana wao wasomi ambao waliaminika katika kuendesha benki hiyo lakini hivi sasa wameshindwa kuiendesha kutokana na kutanguliza mbele maslahi yao binafsi.


“Mtandao huu wa mashirika yasiyokuwa ya serikali wilayani Mbinga, tumesikitishwa na mfumo uliotumika katika kuiendesha benki ya wananchi Mbinga hatma iliyopelekea benki hii kufilisika na kufungwa”, alisema Luena.

Alisema kuwa kupitia wanachama wa mtandao huo wameiomba serikali na vyombo vyake vya uchunguzi isimamie jambo hilo kwa umakini mkubwa ili hata wateja waliokuwa wa benki hiyo ambao waliweka akiba zao siku ya mwisho waweze kurejeshewa fedha zao ambazo waliweka katika benki ya MCB.

Katibu huyo wa MBINGONET alidai kuwa inashangaza kuona benki hiyo jinsi gani ilivyokuwa ikiendeshwa bila kufuata taratibu za kibenki huku akiongeza kuwa idara ya mikopo ndiyo waliosababisha kushindwa kusonga mbele kwa benki hiyo kutokana na kile alichodai kuwa na matumizi mabaya ya fedha ambapo wakati mwingine walikuwa wakitumia fedha pasipo misingi muhimu ya uendeshaji wa benki.

Alifafanua kuwa matumizi ya uendeshaji wa benki kuwa makubwa huku wasimamizi husika wakijua kwamba hawaendeshi kwa faida na mwelekeo kwa baadhi ya watumishi wa benki kujiingizia fedha nyingi katika akaunti zao kwa njia ya mikopo nalo tatizo hilo limechangia kudorola kwa benki hiyo.

Kwa upande wao nao baadhi ya wateja wa MCB kwa nyakati tofauti waliongeza wakidai kuwa hata magari yao binafsi wakati mwingine walikuwa wakitumia fedha za benki hiyo kununulia mafuta na kuweka kwenye magari hayo pasipo sababu yoyote ile ya msingi kufanya hivyo.

“Pia tulikuwa tukiona wakilazimisha kuchukua fedha za benki kununulia vifaa mbalimbali wakati mahitaji ya msingi hakuna, kama vile wanaandikia fedha nyingi kwa ajili ya kununulia vifaa vya stationary wakati mwingine havihitajiki, sisi tulipokuwa tukihoji kwa nini wanafanya hivi tulikuwa tunaonekana wabaya,

“Wakati mwingine wanaingia mikataba ya kihuni na makampuni wanayoyajua wao kwa ajili ya kuchapa kalenda za kila mwaka za benki, utakuta uchapaji wa kalenda hizi wanaandikia idadi kubwa kwamba wamechapa kalenda kwa mfano 2,000 wakati kumbe kalenda walizochapa hazijafikia idadi hiyo na hapa lengo lao ni kutafuta mbinu ya kuiba fedha za benki”, walisema.

Pamoja na mambo mengine, Benki Kuu imeiweka MCB chini ya mfilisi na kuiteua Bodi ya bima ya amana kama mfilisi, kuanzia Mei 12 mwaka huu na kwamba uamuzi huo pia umechukuliwa baada ya BOT kujiridhisha kuwa MCB inaupungufu mkubwa wa mtaji na ukwasi kinyume na matakwa ya sheria ya mabenki na taasisi za kifedha ya mwaka 2006 na kanuni zake.

BOT wakati wanaifunga benki hiyo na kuifutia leseni yake walieleza kuwa upungufu huo wa mtaji na ukwasi unahatarisha usalama wa sekta ya fedha, hivyo kuendelea kwake kutoa huduma za kibenki kunahatarisha pia usalama wa amana za wateja hao.

Vilevile Benki Kuu ya Tanzania imeuhakikishia umma kwamba itaendelea kulinda maslahi ya wenye amana katika mabenki kwa lengo la kutetea ustahimilivu katika sekta ya fedha ambapo imechukua uamuzi huo wa kuifunga Benki ya Wananchi Mbinga kwa mujibu wa kifungu cha 56 (1) (g), 56 (2) (a), (b) na (d), 58 (2) (i), 11 (3) (j), 61 (1) na 41 (a) cha sheria ya mabenki na taasisi za fedha ya mwaka 2006.


Hata hivyo BOT imewataka wale wote wenye amana, wadai na wadaiwa wa iliyokuwa MCB kuwa wavumilivu wakati mfilisi kwa wakati muafaka atawafahamisha wenye amana, wadai na wadaiwa utaratibu wa malipo wa madai, ulipaji wa madeni na taratibu nyingine zitakazohitajika kwa mujibu wa sheria.

No comments: