Wednesday, August 12, 2015

CUF YATAMBA MAJIMBO YA TUNDURU KASKAZINI NA KUSINI


Wagombea ubunge kwa tiketi ya Chama Cha Wananchi CUF, Sadick Songoni kushoto wa jimbo la Tunduru kusini na Manjoro Kambili Tunduru kaskazini, wakiwapungia mkono wananchi wa Tunduru mjini wakati walipokuwa wamewasili kwenye viwanja vya baraza la Idd mjini hapa. 
Na Steven Augustino,
Tunduru.

CHAMA cha wananchi (CUF) wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, kimewataka wananchi wake kujipanga na kuweza kufanya mageuzi ya viongozi katika uchaguzi mkuu ujao Oktoba 25 mwaka huu wa kumchagua diwani, mbunge na Rais.

Katibu wa chama hicho wilaya ya Tunduru, Abdalah Rajabu Abdalah alisema hayo alipokuwa akiwatambulisha wagombea wa ubunge jimbo la Tunduru Kaskazini, Manjolo Kambili na kwa upande wa Tunduru Kusini, Sadick Songoni aliyeteuliwa na chama hicho kupeperusha bendera kwenye jimbo hilo.

Huku akishangiliwa na maelfu ya wananchi ambao walihudhuria kwenye mkutano huo, uliofanyika viwanja vya baraza la Idd mjini hapa, Abdalah alisema kuwa chama hicho kimechukua jukumu la kuwatambulisha wagombea hao ili wanachama waweze kuwafahamu, kabla ya kuanza kwa mpambano wa kampeni Agosti 22 mwaka huu.


Akijitambulisha mbele ya umati wa watu waliokusanyika kwenye mkutano huo, mgombea ubunge jimbo la Tunduru Kaskazini, Manjolo Kambili aliwataka wananchi kujipanga kikamilifu na kufanya mageuzi ya kweli katika uchaguzi huo.

“Ndugu zangu mwaka huu hatuna pingamizi katika kufanya mabadiliko, tunachotakiwa hapa tufanye mabadiliko ya kweli tuwang’oe hawa wabunge wa Chama Cha Mapinduzi”, alisema Kambili.

Naye Sadick Songoni aliyeteuliwa kupeperusha bendera jimbo la Tunduru Kusini alipokuwa akiwasalimia wananchi, mbali na kuwepo kwa ukweli kwamba anacho kibarua kigumu cha kumng’oa Daimu Mpakate (CCM), akiwa anatumia sauti ya katibu mkuu wa CUF taifa, Maalim Seif alitamba kuwa atamgaragaza mgombea huyo.

Wagombea hao walifafanua kuwa katika mchakato wa kampeni hizo, wamejipanga kuwaeleza wananchi mambo mengi ya ufisadi yaliyofanywa na viongozi wa chama tawala, katika nchi hii tangu ipate uhuru miaka 54 iliyopita.

Akifunga mkutano huo Mwenyekiti wa chama cha wananchi CUF wilaya ya Tunduru, Abdalah Mtalika alisema endapo wananchi wa wilaya hiyo hawatabadilisha viongozi wa CCM katika majimbo hayo, na kuweka viongozi kutoka vyama vya upinzania hawataweza kusonga mbele kimaendeleo.

No comments: