Wednesday, August 12, 2015

WATATU WAFARIKI DUNIA BAADA YA KUGONGANA NA LORI

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela.
Na Steven ASugustino,
Tunduru.

WATU watatu ambao ni wakazi wa mtaa wa machinjioni mjini Tunduru mkoani hapa, wamefariki dunia katika ajali iliyohusisha pikipiki waliyokuwa wamepanda baada ya kugongana na lori.

Mashuhuda wa tukio hilo walieleza kuwa ajali hiyo, ilitokea kijiji cha Chingulungulu nje kidogo ya mji wa Tunduru.

Imeelezwa kuwa chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi aliokuwa nao mwendesha pikipiki, ambaye alianguka ghafla mbele ya lori wakati akijaribu kupita.

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela alisema wanamshikilia dereva wa lori hilo anayefahamika kwa jina la Hassan Chimgege, ambaye alijisalimisha polisi baada ya tukio hilo.

Msikhela aliwataja waliopoteza maisha kwamba ni wachimbaji wa vito, ambao walitambulika kwa majina ya Peter Nyange na mwingine kwa jina la Dotho Msukuma ambaye alikwenda mjini Tunduru, kwa lengo la kutafuta maisha katika machimbo hayo.


Kadhalika mwingine aliyefariki katika ajali hiyo ni dereva wa pikipiki hiyo, Yusuph Adam (30) na kwamba watu hao walikuwa wakitokea katika machimbo yaliyopo mto Muhuwesi, wakielekea mjini humo kwa ajili ya kuuza madini hayo ya vito.

Katika tukio hilo lori lenye namba za usajili T 669 ADV mali ya Anton Onesmo mkazi wa mjini hapa, liliwagonga wapanda pikipiki hao ambao nao walikuwa wakisafiria pikipiki yenye namba za usajili MC 703 ABV na kusababisha vifo vyao papo hapo.

Mganga wa Hospitali wilaya ya Tunduru, Dokta Titus Tumbu aliyeifanyia uchunguzi miili ya marehemu hao alibainisha kuwa chanzo cha vifo vyao kilitokana na kutokwa na damu nyingi sehemu mbalimbali, baada ya kukumbwa na mkasa huo.


Dokta Tumbu alifafanua kwamba marehemu Adam alipasuka fuvu la kichwa na Peter alivurugika viungo vya ndani ya mwili wake, huku Dotho akisagika mbavu zake zote kutokana kukanyagwa na magurumu ya gari hilo.

No comments: