Monday, May 30, 2016

DED MBINGA APONGEZWA KWA KUCHUKUA HATUA YA KUDHIBITI MAPATO YATOKANAYO NA MKAA WA MAWE



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

BAADHI ya wananchi wanaoishi katika kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wamempongeza Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo Venance Mwamengo kwa kuchukua hatua ya kufunga mashine ya kukusanyia ushuru katika eneo la Amani Makolo, ambalo husafirishwa mkaa wa mawe kwenda nje ya wilaya hiyo kitendo ambacho kwa kiasi kikubwa kimesaidia kudhibiti mapato ya fedha yatokanayo na mkaa huo.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Walisema kuwa hapo awali kabla ya kufungwa kwa mashine hiyo ya Electronic (EFD’S) mapato mengi yalikuwa yakipotea kutokana na kukusanywa kwa njia ya vitabu vya risiti, ambapo watendaji waliokuwa wakipewa dhamana ya ukusanyaji wa fedha hizo za ushuru walikuwa hawawajibiki ipasavyo.

Theodosia Mahundi mkazi wa kijiji hicho aliwaeleza waandishi wa habari kuwa udhibiti huo wa mapato unapaswa kufanywa kwa kutumia mashine hiyo, katika kila eneo ambalo serikali inakusanya mapato ili kuweza kudhibiti mianya ya wajanja wachache, ambao wamekuwa wakitafuta njia za ufujaji wa fedha za serikali.

Mahundi alisema kuwa ni faraja kwao kuona mapato hayo jinsi yanavyodhibitiwa na kwamba wanaimani kuwa hata serikali, itaweza kuwahudumia wananchi wake kwa kuwapelekea huduma muhimu kama vile madawa kwenye zahanati na vituo vya afya kwa wakati.

Naye Renatus Mapunda mkazi wa kijiji cha Amani Makolo kata ya Amani Makolo alisema kuwa hapo awali madereva wengi wanaosafirisha mkaa wa mawe kwenda nje ya wilaya hiyo, ameshuhudia wakiwa wanakwepa kulipa ushuru huo ambapo alitoa ushauri kwa kuitaka serikali kuendelea kuongeza nguvu ya udhibiti wa mapato yatokanayo na mkaa huo, ili jamii iweze kunufaika nayo kwa njia ya kuwaletea maendeleo katika nyanja mbalimbali.


Kwa upande wake Ofisa anayedhibiti mapato yatokanayo na ushuru wa mkaa wa mawe wilaya ya Mbinga, Justine Ambrose alieleza kuwa mashine hiyo ya EFD’S ilifungwa katika eneo hilo Februari 24 mwaka huu kwa lengo la kuleta ufanisi wa kazi husika.

Ambrose alibainisha kuwa hivi sasa ukusanyaji wake umekuwa mzuri ambapo kila gari linalosafirisha mkaa hutozwa shilingi 30,000 na kwamba kwa siku zaidi ya magari 30 yamekuwa yakilipa ushuru.

“Hapo awali madereva hawa wanaosafirisha mkaa huu wa mawe walikuwa wakitunyanyasa kwa kututolea lugha chafu, wakati mwingine walikuwa wakikimbia kwa lengo la kutaka wasilipe ushuru lakini tumeweza kufanya jitihada ya kuwadhibiti kikamilifu”, alisema Ambrose.

Hata hivyo aliishauri serikali kuweka utaratibu kwa kuwatoza faini madereva wanaokwepa kulipa ushuru pale wanapokamatwa, ili iweze kuwa fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

No comments: