Saturday, May 14, 2016

WAZAZI NAMTUMBO WATAKIWA KUPELEKA WATOTO WAO SHULE



Na Steven Augustino,
Namtumbo.

WAZAZI wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma, wameshauriwa kupeleka watoto wao katika Chuo cha ualimu cha ushirika kilichopo wilayani humo, ili waweze kupata elimu ambayo itawakomboa katika maisha yao, hatimaye wataweza kuondokana na umaskini.

Mkuu wa chuo hicho, Wallfram  Mpulo  alisema hayo katika mahafali ya kwanza ya wahitimu wa ualimu ngazi ya cheti daraja la tatu A, tangu kilipoanzishwa mwezi Julai mwaka 2014 wilayani humo.

“Wazazi msiogope kuleta wazazi wenu katika chuo hiki, leteni vijana wenu wasome hapa shuleni na waweze kujipatia elimu itakayowasaidia katika maisha yao, chuo hiki kimesajiliwa na wizara husika na kinatambulika kisheria”, alisema.


Mpulo alisema kuwa baada ya kuanzishwa kwa chuo hicho, uongozi ulifuata taratibu na kufanikiwa kusajiliwa na  Wizara ya  elimu na mafunzo ya ufundi na kupewa namba usajili CU 142 ya Juni 17/2014 na Septemba 8/2015 kilipata namba ya  usajili wa mtihani  REG/TLF/128P chini ya Baraza la mtihani la Taifa (NACTE).

Alisema ameamua kuvunja ukimya huo, ili kuondoa dhana iliyojengeka miongoni mwa wananchi wa wilaya hiyo kwamba chuo hakijasajiliwa jambo ambalo sio la kweli na limekuwa likiwafanya vijana wa eneo la wilaya ya Namtumbo, kuacha kujitokeza  kuomba kusoma chuoni hapo na kufanya vijana  wengi wanaosoma hapo wanatoka maeneo ya mbali  na wilaya hiyo.

Kufuatia hali hiyo aliwataka wananchi hao kuondoa dhana  hiyo potofu, na kwamba chuo  hicho kimesheheni  wakufunzi  wazuri na wazoefu  wa  kufundisha mambo kisheria  kadiri ya taratibu za wizara zinavyotaka.

Naye Mkurugenzi  na mmiliki wa chuo hicho, Awadhi  alisema  kuwa  aliamua kutumia  fedha  yake  ya pensheni  ya utumishi serikalini  katika  kuhakikisha  anaanzisha  chuo hicho kwa lengo  la  kuhakikisha  vijana  wa Namtumbo, wanapata fursa ya kusoma  ualimu.

Mgeni  rasmi katika  mahafali hayo Ofisa maendeleo ya jamii wilaya ya Namtumbo Martin Mtani, ambaye alimwakilisha Mkuu wa wilaya hiyo Chande  Nalicho  pamoja na mambo mengine alimpongeza Mkurugenzi  wa chuo hicho kwa kujitoa kukianzisha, kwa kutumia fedha yake ikiwa ni lengo la kuendeleza taaluma katika jamii.

Kadhalika Mtani alitoa mwito kwa wananchi wa wilaya hiyo na wilaya zingine hapa  nchini,  kutumia fursa hiyo iliyoletwa na mwenyeji wa wilaya ya Namtumbo kujiunga  katika chuo hicho ili waweze kuendeleza vipaji vyao.

No comments: