Sunday, May 15, 2016

TUNDURU WAMUOMBA MAGUFULI KUTATUA KERO YA MGOGORO WA ARDHI

Rais John Pombe Magufuli.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

SERIKALI imeombwa kuingilia kati na kutafuta ufumbuzi juu ya mgogoro wa mashamba ambao unaendelea kufukuta katika kitongoji cha Ndiyomana kilichopo kijiji cha Msinji kata ya Ligoma wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, kati ya wakulima na wageni wa kutoka shirika la WWF ambao hufanya uwekezaji wa utunzaji wa misitu na ufugaji wa wanyama wilayani humo.

Mgogoro huo ambao umedumu kwa muda mrefu sasa na kufikia hatua ya kuwa kero kwa wananchi wa kitongoji hicho, wamemwomba Rais John Magufuli kuingilia kati na kuweka msimamo ambao utaweza kumaliza kero hiyo.

Wakulima zaidi ya 690 ndio wanaolalamikia juu ya hali hiyo baada ya wageni wa hao kupora ardhi yao huku uongozi wa wilaya ya Tunduru licha ya kupelekewa kero hiyo mezani, bado haijaona umuhimu wa kusikiliza kilio chao na kuchukua hatua za haraka dhidi ya malalamiko ya wakulima hao.


Wakifafanua juu ya suala hilo, walisema mwaka 2015 kijiji cha Msinji kilipokea wageni kutoka kwenye shirika hilo la WWF wenye lengo la kutaka kuanzisha miradi katika hifadhi, lakini wananchi wa kijiji hicho hawakushirikishwa jambo ambalo linawafanya wakose haki zao za msingi.

Pia walisema kutokana na uroho wa fedha na ubinafsi wa  uongozi wa kijiji hicho uliamua kuchukua maamuzi yao pekee yao, bila kuwashirikisha kwa kugawa eneo la wakazi wa kitongoji cha Ndiyomana ili liweze kuwa eneo la hifadhi, kitendo ambacho kimeelezwa kuwa ni cha unyanyasaji dhidi yao.

“Baada ya kubaini kitendo hiki ni cha unyanyasaji, tulichukua hatua ya kufikisha kilio hiki katika ngazi ya wilaya ambapo kwa muda mrefu sasa tumekuwa tukisubiri majibu hakuna mafanikio au utekelezaji wowote uliofanyika”, walisema.

Miongoni mwa waliolalamikia hali hiyo na kumtaka Rais Magufuli aingilie kati ni Seleman Sharif, Omar Juma, Jafari Mnuma na Athuman Bilahi walisema kuwa endapo serikali haitachukua hatua za makusudi za kuutatua mgogoro huo mapema, ipo hatari ya kuzuka kwa ugomvi kati yao na wawekezaji hao wa WWF.

Walieleza kwamba wanaiomba serikali isikilize kilio chao ambacho hivi sasa wameshindwa kupata suluhisho la kudumu, kutoka kwa uongozi wa wilaya ya Tunduru.


Jitihada za kumpata Mkuu wa wilaya hiyo, Agnes Hokororo zilishindikana kutokana na kuwa safarini kwa shughuli za kikazi ambapo mwandishi wetu alifanikiwa  kuongea na Ofisa tawala wa wilaya ya Tunduru, Ghaib Lingo ambaye alikiri kuwepo kwa malalamiko hayo huku akiahidi kuunda tume ya kushughulikia swala hilo.

No comments: